Tuesday 29 March 2016

[wanabidii] Uhakiki wabaini wafanyakazi hewa 1,680

RAIS John Magufuli amesema kuwa uhakiki mdogo uliofanywa hivi karibuni kuhusu tatizo la wafanyakazi hewa nchini, umebaini wafanyakazi hewa 1,680 waliokuwa wakilipwa Sh bilioni 1.8. Amesema ni matarajio kuwa uhakiki unaofanywa nchi nzima utaisaidia serikali kubaini wafanyakazi hewa wengi zaidi na kunusuru fedha nyingi zaidi za Watanzania.

Machi 15, mwaka huu wakati akiwaapisha Wakuu wa Mikoa, Rais Magufuli alitoa siku 15 kwa viongozi hao kuhakikisha wanajumuisha wafanyakazi wote na kuwaondoa watumishi hewa.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja
wa Shule ya Sekondari Chato mkoani Geita jana, Rais Magufuli alitolea mfano wa mfanyakazi mmoja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambaye alikuwa akilipwa mishahara ya watu 17, na kueleza kuwa mfanyakazi huyo atafikishwa mahakamani.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu, Rais Magufuli pia alisema serikali yake imejiandaa kuboresha maslahi ya wafanyakazi kwa kupunguza kodi kutoka asilimia 11 ya sasa hadi asilimia 10 au 9 kuanzia bajeti ijayo.

Lakini alisema kwa wale wanaolipwa mishahara mikubwa, ambayo inafikia hadi Sh milioni 40, itapunguzwa na kuweka kima cha juu cha mshahara usiozidi Sh milioni 15. Rais Magufuli ambaye amefika nyumbani kwake katika Kijiji cha Mlimani, Wilaya ya Chato kwa mara ya kwanza tangu achaguliwe kuwa Rais, alitoa mwito kwa kila Mtanzania kuchapa kazi kwa juhudi ili nchi iondokane na utegemezi wa misaada ya wafadhili ambayo huambatana na masharti.

Dk Magufuli alisema jukumu kubwa lililo mbele ya Watanzania kwa sasa, ni kushikamana na kujisimamia katika maendeleo ili kila mmoja ahakikishe anaongeza uzalishaji na utendaji kazi mahali pake pa kazi.

"Kwa hiyo ni lazima tujisimamie sisi wenyewe, na tukijisimama sisi wenyewe kwa kila mmoja kuwajibika mahali alipo, kama ni mfanyakazi afanye kazi kwelikweli, kama ni mkulima afanye ukulima wake kwelikweli, kama ni mfanyabiashara afanye biashara kwelikweli, kama ni mfugaji afuge kwelikweli, kama ni mvuvi avue kwelikweli, Tanzania hii tutavuka," alisema Rais Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli alisema serikali yake imeamua kuchukua hatua kudhibiti nidhamu serikalini, kwa kuhakikisha inawachukulia hatua watumishi wa umma wanaolisababishia taifa upotevu mkubwa wa fedha, na ameahidi kuwa hatua hizo maarufu kwa jina la "kutumbua majipu" zitaendelea kuchukuliwa hadi tatizo hilo likomeshwe.

Dk Magufuli pia alikumbusha viongozi wote wakiwemo Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala na Wakurugenzi, kutekeleza wajibu wao ipasavyo na ameweka bayana kuwa mahali popote ambapo hapatakuwa na ufanisi, kiongozi husika atakuwa amedhihirisha kuwa hatoshi kuendelea na wadhifa aliopewa.

Rais Magufuli aliwapongeza walimu kote nchini kwa kufanya kazi nzuri ya kufundisha, licha ya changamoto ya ongezeko kubwa la wanafunzi waliojiunga darasa la kwanza mwaka huu, lakini ametaka wazazi na kamati za shule kushirikiana na walimu kuwasimamia wanafunzi ili wafanye vizuri katika masomo yao.

"Naziomba kamati za shule zote Tanzania nzima, kama haziwezi kusimamia
nidhamu ya wanafunzi shuleni, zile kamati za shule zijiuzulu. Lakini pia kama wewe ni Mwalimu Mkuu, shule yako kila siku inatoa divisheni ziro nyingi kila mwaka, sioni sababu ya wewe kuendelea kuwa Mwalimu Mkuu," alisisitiza Dk Magufuli.

0 comments:

Post a Comment