Thursday 27 November 2014

[wanabidii] Uenyekiti wa EAC kuchukuliwa na Tanzania

Mkutano wa 16 wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utafanyika Tarehe 30 Novemba, 2014 Nairobi, Kenya. 

Kwa mujibu wa Mkakaba Mkutano huu utatanguliwa na Mkutano wa Baraza la Mawaziri la
Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika Tarehe 20 – 27 Novemba, 2014 katika ngazi ya Wataalam, Makatibu Wakuu na Mawaziri. Aidha, katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatarajiwa kukabidhiwa uwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kipindi cha mwaka mmoja na Jamhuri ya Kenya inayomaliza kipindi chake, Ikiwa ni utekelezaji wa Ibara ya 12 (2) ya Mkataba wa Uanzishaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Akizungumzia Tanzania kuchukua Uenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Katibu Mkuu wa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Joyce Mapunjo alisema, "Katika kipindi cha uenyekiti wake, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendeleza mafanikio yaliyopatikana wakati wa kipindi cha uenyekiti wa Jamhuri ya Kenya. Aidha, mkazo utawekwa katika kuhakikisha mtangamano wa Afrika Mashariki unaendelezwa kwa kuzingatia matakwa ya Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya pamoja na Kanuni na Taratibu za Jumuiya. Aidha, mkazo utawekwa katika kuhakikisha Sekta binafsi na Wadau wengine wanashirikishwa kikamilifu katika utekelezaji wa mtangamani wa Afrika Mashariki ikiwa ni pamoja na kuzitumia fursa zitokanazo na Jumuiya ya Afrika Mashariki,"

Mkutano wa 16 wa Wakuu wa Nchi utatanguliwa na Mkutano wa tatu wa Kazi wa Wakuu wa Nchi kuhusu uendelezaji wa miundombinu katika Jumuiya. Mkutano hu utapokea taarifa ya utekelezaji wa maagizo waliyoyatoa katika mkutano wa pili uliofanyika mwezi Novemba, 2012 na kuidhinisha miradi 72 ya miundombinu ya kipaumbele ya barabara, reli, nishati na bandari. Kwa upande wa utekelezaji miradi 16 imekamilika, 39 utekelezaji unaendelea na 17 ipo katika hatua za awali za kutafutiwa fedha kwa ajili ya utekelezaji wake.

Kwa upande wa Tanzania miradi nine imekamilika ambayo ni kuupatia mji wa Kibondo umeme, mradi wa barabara ya Mbezi-Shule-Tangibovu-Makutano ya Nelson Mandela na barabara ya Tabata. Barabara nyingine iliyokamilika ni Nyangunge – Musoma-Airari. Shemu ya Simiyu-Musoma inayounganisha Kenya na Tanzania ujenzi unaendelea.

Kwa mujibu wa Agenda, Wakuu wa Nchi watapokea taarifa ya Baraza la Mawaziri la Jumuiya kuhusu utekelezaji wa mtangamano wa Afrika Mashariki kwa kipindi cha Novemba, 2013 – Novemba, 2014. Aidha, Wakuu wa Nchi watajadili hatua iliyofikiwa katika majadiliano ya Sudan Kusini kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki, maombi ya Jamhuri ya Somalia kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki, suala la uchangiaji katika bajeti ya Jumuiya na mapitio ya mfumo wa Kitaasisi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. 

Wakuu wa Nchi watajadili pia hatua iliyofikiwa katika majadiliano ya uanzishaji wa Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki Ikiwa ni pamoja na maandalizi ya Mpangokazi wa kuelekea katika Shirikisho pamoja na mchakato wa kuiongezea mamlaka Mahakama ya Afrika Mashariki ili iweze kushughulikia mashauri yanayohusu biashara, uwekezaji na utekelezaji wa Umoja wa Fedha wa Afrika Mashariki.

Kumekuwepo na mafanikio kupitia ushiriki wa Tanzani katika Jumuiya ya Afrika Mashariki. Tangu kuanza kwa Umoja wa Forofha wa Afrika Mashariki, mauzo ya Tanzania katika Jumuiya ya Afrika yameongezeka kutoka Dola za Marekani Milioni 142 mwaka 2005 hada kufikia Dola za Marekani Milioni 1,120 mwaka 2013. Bidhaa ambazo zimekuwa zikiuzwa kwa wingi ni pamoja na nafaka, karatasi, mbole, vifaa vya umeme, mashine, bidhaa za mafuta na vimiminika, vyandarua, bidhaa za plastiki, chai, na bidhaa za karatasi. Bidhaa nyingine ni saruji, matunda, chuma, samaki, ngano, sukari na nguo. 

Kwa upande wa uwekezaji, miradi iliyowekezwa hapa Nchini kutoka nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki imeongezeka kutoka miradi 35 yenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 39.65 mwaka 2005 na kufikia Miradi 244 yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 676.45 mwaka 2013. Miradi hii imezalisha jumla ya ajira 15,721 katika kipindi husika. 

Katika kuimarisha biashara na fursa za masoko ndani ya Jumuiya, Tanzania imeanza utekelezaji wa mfumo wa Himaya ya Forodha ulioanza 1 Julai, 2014. Katika mfumo huu, uthamini wa bidhaa na ukusanyaji wa kodi unafanyika katika Nchi mwanachama iliyoagiza bidhaa na baada ya kuthibitisha kwamba kodi imelipwa bidhaa zinaondolewa kutoka bandari ya Dar es salaam na kusafirishwa kwenda nchi husika mwanachama chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Forodha kwa kutumia mfumo wa Kieletroniki wa Ufuatiliaji wa bidhaa. Aidha, bidhaa zilizolipiwa kodi katika Nchi husika husafirishwa hazihitaji kuwekewa dhamana na hivyo kupunguza gharama za kufanya biashara.

Kwa upande wa uendelezaji wa Miundombinu Jumuiya imeandaa Mipango Kabambe ya uendelezaji wa barabara na reli zinazounganisha Nchi Wanachama. Utekelezaji wa mipango hiyo unaendelea na kwa upande wa Tanzania umehusisha ujenzi wa barabara ya Arusha- Namanga-Athi river, Arusha-Holili-Voi-Mwatate na Malindi-Lingalinga lunga/Tanga-Bagamoyo zote zikiunganisha Tanzania na Kenya. Kwa upande wa mtandao unaounganisha Tanzania, Burundi, Rwanda na Uganda ujenzi wa barabara zinazoanzia Tunduma-Iringa/Sumbawanga na kuelekea nchi hizo jirani umekamilika.

Ibara ya 124 ya Mkataba inatambua kuwa amani na usalama ndiyo msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Jumuiya ya Afrika Mashariki. Nchi Wanachama zimeidhinisha na kutekeleza Mkakati wa kikanda wa Amani na Usalama tangu mwaka 2006. 

Katika kukabiliana na changamoto za kiusalama katika Jumuiya Mkakata huu umefanyiwa mapitio na kuongeza masuala ya Kukabiliana na Uharamia, Kupambana na uhalifu wa kimtandao, Biashara Haramu ya Usafirishaji wa Binadamu, Mauaji ya Kimbari na Usafishaji wa fedha haramu ambazo ndizo zimekuwa zikitumika kufadhili uhalifu. 

Aidha, ili kushirikisha wadau zaidi katika kuimarisha usalama, Jumuiya iliandaa kongamano la viongozi hao katika kuzuia kusambaza kwa waumini wa itikadi kali za kidini na pia kuwashirikisha katika kufundisha umuhimu wa imani yao ya dini na amani kwa waumini wao. Katika kuhakikisha wanachi wanashirikishwa utaratibu wa Katibu Mkuu wa Jumuiya kukutana na Sekta binafsi, Asasi za kiraia na wadau wengine kwa ajili ya mashauriano na kupata maoni yao juu ya uendeshaji wa Jumuiya. 

Imetolewa na 
Katibu Mkuu

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.

0 comments:

Post a Comment