Tuesday 4 December 2012

[wanabidii] Kongamano Disemba Tarehe 9 Nkrumah, Chuo Kikuu

UNIVERSITY OF DAR ES SALAAM
Academic Staff Assembly
 
 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 4/12/2012
 
 
Ndugu Waandishi wa Habari,
 
Kwanza kabisa tunapenda kuchukua fursa hii kuwashukuru kwa mwitikio wenu wa kuja kuzungumza nasi leo. Lengo la kuwaalika katika mazungumzo haya ni kutaka kuwapeni taarifa kuhusu Kongamano ambalo Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDASA) limeandaa.
 
Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakiwa sehemu ya watanzania, wamekuwa wakitafakari historia ya taifa letu tangu tulipopata uhuru tarehe 9 Desemba 1961. Mwaka jana 2011 tulifikisha miaka 50 ya uhuru na mwaka huu tunaanza rasmi safari ya miaka mingine 50. Tukiwa kama taifa moja, tumeona kwamba ipo haja ya kutafakari tulikotoka, jinsi tulivyojiongoza na kujiendesha kama taifa huru kwa miaka yote hamsini, na pia ni fursa ya kutafakari wapi tumekosea na wapi tumefanya vizuri kama taifa ili tuweze kujenga upya mustakabali wa taifa letu kwa miaka 50 ijayo.
 
Kwahiyo, UDASA tumeamua kuandaa kongamano siku ya tarehe 9 Desemba kwaajili ya kujadili mustakabali wa taifa letu. Mada kuu ya kongamano hilo ni "Uhuru Wetu na Mustakabali wa Taifa kwa Miaka 50 Ijayo". Katika Kongamano hilo tunalenga kuwa na mada ndogo tatu ambazo washiriki watazijadili, nazo ni:
a)      Amani na Utulivu wa Taifa Letu kwa Miaka 50 Ijayo;
b)      Elimu Yetu na Maendeleo ya Taifa kwa Miaka 50 Ijayo;
c)      Rasilimali Zetu na Maendeleo ya Kiuchumi ya Taifa.
 
Kongamano hilo litafanyika kuanzia saa 8 mchana hadi saa 12 jioni. Kwa bahati nzuri tuliweza kuongea na kituo cha Televisheni cha ITV, Radio One na Capital Radio wawe washirika wetu katika kongamano hili, na kwa bahati nzuri wamekubali kurusha moja kwa moja matangazo ya kongamano hilo. Tunawashukuru sana kwa ushirikiano wao kwetu na kwa taifa zima.
 
Tunatarajia Mgeni Rasmi atakayefunga kongamano hilo ni waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ndugu Bernard Membe (MB). Tunatarajiwa kuwa na wazungumzaji wakuu watakaongoza mijadala hi hawa wafuatao:-
 
i)                    Prof. Gaudence Mpangala na mwandishi maarufu Maggid Mjengwa. Hao wataongoza mjadala kuhusu Amani na utulivu wa nchi yetu.
ii)                  Dkt. Martha Qorro, na Dkt Kitila Mkumbo wataongoza mjadala kuhusu Elimu na maendeleo ya taifa letu.
iii)                Pia tutakuwa na Mhandisi Joshwa Raya na Dkt Haji Semboja ambao wataongoza mjadala kuhusu Rasilimali za taifa na Maendeleo ya kiuchumi ya taifa letu.
iv)                Mbali na hawa wazungumzaji wakuu, pia tumewaalika wachangiaji wengine ambao nao tunatarajia kuwapa nafasi ya kuzungumza. Pia tunategemea kuwa na wachangiaji kutoka vyama vya siasa kama vile CCM. Chadema na CUF ambao wameonyesha nia ya kufika, ambao ni Ndugu Januari Makamba (Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia), Julius Mtatiro atakayewakilisha CUF na Bi. Esther Wassira atakayewakilisha Chadema. Mbali na hao, pia tumeaalika watu mbalimbali kutoka taasisi za serikali, wizara, na mashirika binafsi nk kama vile Mzee Joseph Butiku, Dkt Aldin Mutembei (TATAKI), Bi. Usu Mallya (TGNP, Ndugu Deogratias Filikunjombe (Mbunge wa Ludewa).  
 
Dhamira yetu kuu ya kuandaa kongamano hili ni kuchochea mjadala endelevu kuhusu mustakabali wa taifa letu. Kwa sasa tumechagua maswala haya matatu ambayo tunaamini yana athari mtambuka kwasababu kama kutakuwa na Amani ya kweli na utulivu nchini, wananchi watafanya shughuli za kiuchumi kwa mafanikio. Na kama tutakuwa na elimu yenye kumlenga mtanzania kujikomboa basi hata kilio cha ukosefu wa ajira kitapungua na tutaachana na tatizo la kuwa omba omba kwa mataifa tajiri. Pia tunataka kama taifa moja tujadili kuhusu rasilimali zetu na mchango wake katika uchumi wa taifa na kuona kama kweli zinatunufaisha watanzania. Kama rasilimali zetu zitasimamiwa vizuri na kipato chake kutumika kwa manufaa ya kiuchumi ya taifa letu basi tutakuwa na uwezo wa kuwahudumia watanzania wenzetu katika maswala ya afya, ajira, elimu, kilimo nk.
 
Ombi letu kwenu waandishi wa habari na watanzania kwa ujumla ni kwamba kongamano hilo liamshe ari na ujasiri wa watanzania kujadili kuhusu mustakabali wa taifa lao. Tunapenda tuanze kuwaza na kutenda pasipo kusukumwa na matashi ya kisiasa. Mwito wetu kwa watanzania wenzetu ni kuweka siasa pembeni lipofika swala lenye maslahi kwa taifa. Tunaomba watu wajadili kwa uhuru na uwazi kabisa pasipo kubeza mawazo ya wengine kwa kudhani ya kwao ni bora zaidi. Kongamano hili halilengi kukuza mitizamo ya kisiasa bali mitazamo ya kulijenga taifa letu kwa vizazi vijavyo. Tusiwe watu wa kwanza kuliangamiza taifa letu na kuliacha tupu kiasi cha kuhatarisha maisha ya vizazi vijavyo. Tunawaalika watanzania kwa kongamano hilo kwa kufika ukumbini au kwa kufuatilia kupitia ITV, Radio One na Capital Radio.
 
Wito wetu kwenu waandishi wa habari na vyombo vya habari ni kutumia kongamano hili kuibua mawazo yenye tija kwa taifa. Tunaomba muwe wadau wetu wakubwa wa kuendeleza mjadala ili hatimaye sisi kama taifa tupate mfumo utakaoweza kulikomboa taifa letu na umaskini, ujinga, utegemezi, maradhi, na ukuaji wa matabaka ya kiuchumi miongoni mwa watanzania. Waandishi muwatumie wachangiaji wetu ambao kwa bahati mbaya watapewa muda mfupi kusema lakini wanayo hazina kubwa ya mawazo. Watumieni hao kuendeleza mijadala kwenye televisheni zenu, radio zenu na kwenye magazeti yenu ili jamii pana ya kitanzania iweze kunufaika na mawazo yao.
 
Asanteni sana.
 
 
 
 
 
Aldin K. Mutembei   (PhD)                         Aldin Mutembei (PhD)
Mkurugenzi                                                  Director
Taasisi ya Taaluma za Kiswahili                  Institute of Kiswahili Studies
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam                   University of Dar es Salaam, TANZANIA
+255 222 410 757     [Ofisini]                     +255 222 410757 (Day time-Office)
+255 715 426 162      [Kiganjani]                +255 715 426 162  (Cell)
b-pepe: kaimutembei@gmail.com                Alternative e-mail: <kaimutembei@gmail.com>




0 comments:

Post a Comment