Tuesday 26 March 2013

[wanabidii] Dk. Slaa atajwa kumtuma Saanane kummaliza Zitto Kabwe

*Yadaiwa ilipangwa anyweshwe sumu hotelini
*Dk. Slaa atajwa kumtuma Saanane kummaliza
*Mwenyewe akanusha, asema ni siasa chafu

TISHIO la kuuawa kwa Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA), Zitto Kabwe, sasa limechukua sura mpya, baada ya
kuibuika kwa madai mapya kuwa Bosi wake, Dk. Willbrod Slaa, alipanga
njama za kumuangamiza, MTANZANIA Jumatano linaripoti.

Duru za habari zinaeleza kuwa Zitto, ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma
Kaskazini na Naibu Kiongozi wa Upinzani bungeni, anadaiwa alitaka
kuuawa kwa sumu na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Slaa, ambaye
alimtumia kada na Mjumbe wa Baraza la Vijana la Chadema (BAVICHA), Ben
Saanane, kutekeleza mpango huo.

Habari zinadai kuwa tukio hilo lilipangwa kutekelezwa Mei mwaka jana,
katika Hoteli ya Lunch Time, iliyoko Mabibo External, jijini Dar es
Salaam.

Kwamba Zitto alilengwa kuuawa kwa kuwekewa sumu kwenye kinywaji chake
wakati akiwa kwenye mazungumzo na baadhi ya makada vijana wa chama
hicho katika Hoteli ya Lunch Time.

Mmoja wa watu waliokuwa katika tukio hilo amelieleza MTANZANIA
Jumatano kuwa Zitto alinusurika baada ya aliyetumwa kumuwekea sumu
hiyo kuidondosha na hivyo kuonekana kwa watu waliokuwa eneo hilo.

Anamtaja mtu aliyetumwa kumuua Zitto kuwa ni Ben Saanane, ambaye
aliangusha karatasi ya nailoni iliyokuwa na ungaunga unaosadikiwa kuwa
sumu na kuonekana kwa watu waliokuwa eneo hilo, akiwemo Zitto mwenyewe
pamoja na aliyekuwa Naibu Mwenyekiti wa Bavicha, Juliana Shonza na
Mtela Mwampamba.

Akizungumza na MTANZANIA Jumatano, Shonza alikiri kutokea kwa tukio
hilo kwa kueleza kuwa yeye na Mwampamba walihoji kilichokuwa ndani ya
nailoni ile, ambacho kilionekana wazi kuwa ni unga unga ni nini,
ambapo Saanane alikiri kuwa ilikuwa sumu ambayo alipewa na Dk. Slaa,
ili amuwekee Zitto.

Shonza alidai kuwa siku ya tukio, yeye na Zitto walikuwa wamekaa meza
moja na Saanane ambaye mkono wake wa kushoto ulikuwa umefungwa bandeji
aliyowaeleza kuwa aliifunga kutokana na maumivu ya mkono.

Alisema wakiwa katika maongezi, huku Saanane akionyesha kuzidiwa na
kilevi alichokuwa amekunywa, alitoa bahasha ya kaki yenye fedha ili
alipie gharama za vinywaji vya wote ambayo ilidondoka na ndani yake
ikatoka karatasi ndogo ya nailoni ikiwa na unga mwekundu.

Kwa mujibu wa Shonza, Saanane alipobanwa aeleze unga ule ulikuwa nini,
awali alidai ni kilevi aina ya kuberi, huku akiwataka wasiifungue
nailoni hiyo, jambo ambalo Mwampamba alilikataa na kulazimisha
ifunguliwe pale pale.

"Kwa hasira Ben alitaka arudishiwe ile karatasi, lakini, Mwampamba
aliondoka nayo, usiku huo huo Saanane alimtafuta Mwampamba hadi
nyumbani kwake akidai apewe mzigo wake.

"Mwampamba alimwambia atampa mzigo wake kwa sharti moja tu la kusema
ukweli kuhusu kilichomo ndani ya nailoni hiyo na hapo ndipo Ben
alipokiri kuwa alipewa mzigo huo ambao una unga unga wenye sumu na Dk.
Slaa, ili amuwekee Zitto kwa sababu amekuwa akimsakama ndani ya vikao
vya chama.

"Huo ndiyo ukweli ambao nitausema popote, sasa kama Ben alitudanganya
kwa kumsingizia Dk. Slaa hiyo ni juu yao wenyewe," alisema Shonza.

Shonza alisema hali hiyo iliwaogofya na kuanza kuwa makini katika
mapito yao na kuongeza kuwa Zitto bado yuko Chadema kwa sababu ana
roho ngumu, mvumilivu na mkomavu wa kisiasa, anayeweza kukabiliana na
mambo ya hatari.

Dk. Slaa alipoulizwa na MTANZANIA Jumatano kuhusu madai hayo, alisema
hilo ni kosa la jinai, ambalo kama anatuhumiwa kulifanya anapaswa
kushtakiwa kwenye vyombo vya dola badala ya tarifa hizo kupelekwa
katika vyombo vya habari.

"Usipende kutumiwa na watu, lakini aliyekutuma anajua amekutuma kwa
sababu gani. Sasa nitakujibu, hivi suala la kuua si ni jinai? Sasa
suala la jinai linapelekwa kwenye vyombo vya dola au kwenye vyombo vya
habari? Huyo aliyesema yuko Chadema au yuko wapi? Aliyesema hakwenda
polisi? Aliyetaka kuuawa hakwenda pia? Sasa ninyi media mmekuwa nani?

"Wa kumuuliza suala hili ni Saanane mwenyewe au Shonza, wangekuwa na
nia njema wangekwenda polisi au Zitto mwenyewe angekwenda polisi
kushitaki kwa kutaka kuuawa," alisema Dk. Slaa.

Naye Saanane ambaye amefanya mahojiano na MTANZANIA Jumatano kuhusiana
na mambo mbalimbali mabaya ambayo yamekuwa yakielekezwa kwake,
akizungumzia madai hayo alisema madai hayo hayana ukweli wowote, bali
yanaibuliwa sasa na mahasimu wake kisiasa kwa lengo la kutaka
kumshusha baada ya majaribio mengi dhidi yake kushindwa.

"Kwanza siku ambayo wanasema tulikuwa wote mimi sikuwa huko, nashangaa
na haiingii akilini kwamba mimi niende hadi Temeke (kwa Mwampamba)
tena usiku wa manane kwa ajili ya kufuata sumu ya kuulia panya.

"Hizi ndizo siasa halisi za maji taka, kuliko nipange njama za kuua
mtu kwa malengo ya kisiasa, ni bora niache siasa. Ni mwendawazimu
pekee atakayeweza kuamini tetesi hizi za ovyo kabisa zinazofanywa na
vijana walioshindwa kujenga hoja za maana kwenye majukwaa," alisema
Saanane.

Aliwaonya watu wanaohasimiana naye kisiasa kuacha kumchafua Dk. Slaa
kwa kutumia jina lake katika mambo wanayomtuhumu, kwa kile alichoeleza
kuwa ni dhambi kubwa kutunga uongo na kuusambaza ili kutafuta huruma
ya umma wa Watanzania.

"Nadhani lengo lao hapa ni kumchafua Dk. Slaa kwa tuhuma hizi za uongo
zilizotolewa kwa mara ya kwanza na vijana waliotimuliwa Chadema kwa
kukisaliti chama na baadaye kuhongwa na makada na viongozi wa CCM
ambao wamejiunga nao sasa.

"Sasa kwa tuhuma hizo, kwa nini wasiripoti polisi, inaingiaje akilini
mtu kupanga njama kubwa kiasi hicho halafu ukae kimya tu," alisema
Saanane.

http://mtanzania.co.tz/index.php?option=com_content&view=article&id=6419:siri-ya-kuuawa-zitto-yafichuka&catid=25:siasa&Itemid=41

--
Jobs in Africa - www.wejobs.blogspot.com
International Jobs - www.jobsunited.blogspot.com

Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma

Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.

0 comments:

Post a Comment