Friday 30 August 2013

[wanabidii] UCHAFUZI WA MAZINGIRA DAR, MAMLAKA HUSIKA MPO?

Ni juzi tu Mheshimiwa Waziri kutoka wizara inayohusika na mazingira alifanya ziara ya ukaguzi wa mazingira katika jiji la Dar es salaam. Nampongeza sana kwa hilo. Kabla ya hapo, kumekuwepo na kampeni mbalibali kuhamasisha usafi na utunzaji wa mazingira katika miji na majiji yetu zikiongozwa na wiraza ya Afya .Napongeza ndugu zetu JWTZ kwa kuonyesha mfano kwa kampeni yao waliyoifanya katika jiji la Mwanza, kwa kuonyesha kuwa uchafu ni adui asiyeefaa kwa binadamu na anafaa kushughulikiwa ipasavyo na kila mtu, vikiwemo vyombo vya ulinzi na usalama.

Pamoja na juhudi nyingi kufanywa, nasikitika kusema kuwa JIJI la Dar au DSM, kama lilivyozoeleka kuitwa BONGO ni chafu, tena chafu kupindukia. Nimejaribu kuwaza sana nini kifanyike kulinusuru jiji la Dar kutoka kwenye lindi hili la uchafuzi wa mazingira, bado nashindwa kupata jibu. Jiji  la Dar kuna Viongozi wa serikali na  wasomi wengi, wafanyabiashara , matajiri na masikini (wengine huwaita walala hoi). Ni jiji linalotembelewa na watu mbalimbali wakiwemo wageni kutoka nchi za nje. Kukithiri kwa uchafu kunatia aibu kwa jamii na wageni , licha ya madhara ya kiafya yanayoweza kujitokeza kutokana na kukithiri kwa uchafu huu.

Nimejaribu kuwaza na kulitizama jiji la Dar kwa jicho la pili, waswahili husema kuwa kutumia " kiona mbali". Na pia nimejaribu kulinganisha uchafu wa jiji la Dar na miji au majiji mengine kama Moshi, Njombe, Mwanza, Mbeya, Iringa n.k; kiwastani Dar inatisha kwa hali ya uchafu. Baadhi ya watu wanaweza kudhani kuwa ninayoyasema si ya kweli, la hasha; Nakuomba leo hii jaribu kulizunguka jiji la Dar ili uwe shuhuda wa haya niyasemayo. Utakutana na taka zilizozagaa na kutupwa hovyo, mitaro michafu na iliyoziba, madimbwi ya majimachafu kila kona ya jiji karibu na makazi ya watu, utakutana pia na kile usichoweza kukidhania ( malundo ya taka katika barabara zinaojengwa na pembezoni mwa hizo barabara). 
Wakati mwingine unaweza kudhani Dar hakuna Sheria, miongozo na taratibu za uendeshaji wa jiji. La hasha,  viongozi wapo, sheria zipo na taratibu zote zpo, ila tatizo ni usimamiaji na utekelezaji wa sgheria hizi. 

Juzi nikiwa ndani ya usafiri wetu wa kukanyagana ( Daladala ) nikitokea nyumbani Kimara kuelekea  kazini ( Dar ukitaja kazini, unamaanisha maeneo ya city centre, kariakoo na vitongoji vyake) nilishuhudia uchafu uliokithiri ukiwa  umetupwa maeneo ya Faya (fire) kandokando ya ukuta wa shule ya Sekondary Jangwani. Hii ni sehemu iliyowazi, na haistahili kabisa kutupa uchafu na wala  kuchoma taka, lakini Kwa Dar ( Bongo) hiki ni kitu cha kawaida, ukuta unapakwa rangi leo, kesho taka zinachomwa tena pembeni kabisa na ukuta/ fance ya shule  nakuharibu kilakitu na hakuna wa kusema ( kila mtu yupo bize na mambo yake!). Leo barabara inapanuliwa na kujengwa ( morogoro road) pesa za taifa zinatumika katika hili, kesho utakuta miundombinu hii inaharibiwa baadhi ya watu kwa sababu wanaozijua wao ( Hii ndiyo Dar).

Tembelea masoko ya Dar, Kariakoo shimoni ni shimoni kweli, Ilala, Manzese, Vigunguti, Mwananyamala, na kwingineko kwingi utashangaa kukuta malundo ya uchafu na hisia ya  harufu kali. Utashangaa hapa ndipo chakula kinatoka au umekosea ukapita jalalani/dampo. Siku moja nikiwa katika pitapita zangu nilimuuliza babu mmoja juu ya nini kifanyike kuinusuru Dar na uchafu, Babu yule hakusita, akajibu (" Ningekuwa mimi ningemrudisha mkoloni atawale ili  awanyooshe nyie watu wa sikuhizi, mkoloni alikuwa hana mchezo na watu kama hawa wanaovunja sheria. Akikuta uchafu eneo unaloishi au kufanyiakazi, wewe na kiongozi wako wote mnaingia hatiani -" Viboko", baada ya hapo ndiyo mazungumzo yanafuata nini kifanyike" ) . Na kweli nilipotafakari maneno ya babu huyu, nikagundua kuwa viongozi wa  enzi za kikoloni walikuwa wawajibikaji na waliofuta na kusimamia sheria kikamilifu, kwa maana hiyo mambo yote ylienda kama ilivyopangwa,  kitu ambacho siku hizi ni nadra sana. Rushwa na kuoneana haya  na uzembe vimedhoofisha uwajibikaji, matokeo yake yanamadhara makubwa.

Uchafuzi wa mazingira Dar unawezekana kabisa ukutatuliwa ikiwa kila mtu atawajibika ipasavyo kuweka mazingira yanayomzunguka katika hali ya usafi. Sheria zikifuatwa , kusimamiwa na kutekelezwa na mtu mmoja mmoja na mamlaka husika pia, na wananchi wenyewe wabadilike wachukie tabia ya Uchafu na uchafuzi wa mazingira.


Wakunga husema "Tunza mazingira nayo tyakutunze."

0 comments:

Post a Comment