Wednesday 1 May 2013

[wanabidii] Ephata Nanyaro : MALALAMIKO YANGU KWA BARAZA LA UONGOZI LA MKOA DHIDI YA NDUGU GODBLESS LEMA

WILAYA YA ARUSHA MJINI 
P.O.BOX 1225 ARUSHA 
HSE NO.8 
NHC STREET 
NGARENARO 
www.chademaarusha.com 



KATIBU WA MKOA 
CHADEMA MKOA WA ARUSHA 
P.O. BOX 12525 
ARUSHA. 


Mh. Katibu wa Mkoa, 

YAH. MALALAMIKO YANGU KWA BARAZA LA UONGOZI LA MKOA DHIDI YA NDUGU GODBLESS LEMA

Kwanza nitumie fursa hii kutoa salam zangu za dhati kwa chama chetu, ambacho kimejipambanua kuwa chama chenye kufuata Katiba, Kanuni na Maadili ya chama. 

Waheshimiwa wajumbe wa Baraza la Uongozi la Mkoa, kwa muda mrefu sasa ndugu Godbless Lema amekuwa akinituhumu mitaani, kunidhalilisha, kunitukana matusi makubwa ya nguoni na kunikashfu mimi kama Mwenyekiti wa chama wa wilaya na uongozi mzima wa chama wilaya kinyume cha katiba, kanuni na maadili ya chama. Aidha kuna mambo mengi mengine ambayo amekuwa akiyafanya ndani na nje ya chama ambayo ni kinyume na katiba, kanuni na maadili ya chama na ambayo kimsingi yanamkosesha sifa ya kuendelea kuwa si tu kiongozi ndani ya chama bali hata kuwa mwanachama wa chama makini kama CHADEMA. 


Waheshimiwa viongozi, natambua kabisa kwamba kikatiba kwa nafasi aliyonayo Lema ndani ya chama kwa sasa, mashtaka haya yanaweza kabisa kushughulikiwa na ngazi ya wilaya. Lakini kwa kuwa kama nitakavyoonyesha hapa, yako makosa mengi ambayo Lema ameyafanya dhidi yangu binafsi kama mwenyekiti wa chama wilaya, na kwa kuwa kamati ya utendaji ya wilaya ambayo inaweza kushughulikia mashtaka dhidi yake mimi ndiye mwenyekiti wake, na kwa kuwa baada ya kuvumilia kwa muda mrefu nimeshindwa kuendelea kuvumilia anayoyafanya na kwa hiyo katika malalamiko haya mimi nasimama kama mlalamikaji, nimeona suala hili lishughulikiwe na Baraza la Uongozi la Mkoa kwa ajili ya kutenda haki kwa pande zote. 


Sasa naomba kuwasilisha mashtaka yangu dhidi ya Ndugu Lema kama ifuatavyo: 

  1. FUND RISING NA UFUJAJI WA FEDHA YA CHAMA.

Waheshimiwa viongozi, Lema amekuwa akichangisha marafiki wa CHADEMA hela. Anatumia vibaya nafasi ya chama kukubalika sana Arusha kujinufaisha binafsi. Kuna watu wenye uwezo na mapenzi mema kwa CHADEMA na kwa muda mrefu sasa hasa baada ya mwezi wa Machi mara baada ya kuzindua Fundrising iliyofanyika Naura Springs Hotel-Arusha, Lema aliendelea na kukusanya hela kwa marafiki wa CHADEMA bila kushirikisha viongozi wa chama. Amekuwa akitumia jina la chama kukusanya fedha hizo na badala ya kuzisalimisha kwenye chama huzitumia kwa namna ambayo hakuna anayejua na hivyo kujinufaisha yeye mwenyewe, jambo ambalo ni kinyume cha maadili na sifa za viongozi Rejea Kanuni za chama kama zilivyonukuliwa katika Ibara zifuatazo: 
"8.5 Michango yoyote ya hiari kutoka kwa wanachama itapangwa na kuidhinishwa na Kamati za Utendaji za kila ngazi kwa mahitaji ya kila ngazi na katibu mkuu kwa shughuli za kitaifa. 10.1 {v} Kiongozi asitumie wadhifa wake kujinufaisha binafsi au ukoo au familia au rafiki zake…. {vi} Kiongozi anatarajiwa kujitosheleza yeye na familia yake kwa mapato halali na kuepukana na tabia ya kukopa kwa kuzidi uwezo wake au kuwa omba omba kwani tabia hiyo itadhoofisha uwezo wake wa kutoa maamuzi sahihi yasiyo na upendeleo au yanayoegemea kwa wanaompa fadhila….. {vii} Kiongozi anatakiwa kulinda mali zote za chama kwenye ngazi yake na kusimamia matumizi ya mali za chama kwa faida ya chama na wanachama wake. Ni mwiko kwa kiongozi yeyote kutumia mali za chama kwa maslahi binafsi " Fundraising alizofanya ni ile ya Tarehe 18 Novemba 2012 ambapo Lema aliwaita baadhi ya makamanda wetu nyumbani kwake na katika kikao hicho aliwajulisha waliohudhuria kuwa amewaita ili kutoa mchango kusaidia WAGOMBEA ambao tayari walishatangaza nia ya kugombea kwenye majimbo yao. Hela zilikusanywa hapo hapo ambapo Tshs 800,000 (Laki nane) zilipatikana hapo hapo na ahadi ya zaidi ya shilingi milioni 2. Aidha mpaka ninapowasilisha barua hii, anaendelea na maandalizi ya tukio kubwa la fundrising December 15, 2012 ambalo uongozi wa chama ngazi zote kuanzia wilaya hadi matawi hauna taarifa na nina shaka kama uongozi wa mkoa na taifa wanalijua tukio hilo wala makusudio yake ni nini, mbaya zaidi fedha hizi zinakusanywa kwenye Account ya Mtu binafsi lakini kwa kupitia mgongo wa CHADEMA. Viongozi wakuu wa mkoa mtakumbuka nilishawaeleza tukio lingine la mapema mwezi wa sita ambapo alikusanya zaidi ya shilingi 8mil kwenye hotel ya Charity, ambazo alidai kuwa ni kwa ajili ya M4C Simanjaro. Fedha hizo hadi leo hazina mahesabu Wilayani wala kwenye ngazi yoyote ya chama. Viongozi pia mtakumbuka wakati tunasitisha mikutano ya M4C Ngorongoro, yeye aliendelea kukusanya pesa kwa madai ya kufanya mikutano Ngorongoro. Kilichokuja kutushtua ni pale tulipoona namba ya kamanda wetu ndugu Frank Olelesho namba 0766265709 imeandikwa kwenye mtandao wa facebook kwamba ndiyo inayotumika kukusanya michango hiyo. Mheshimiwa Katibu wa Mkoa utakumbuka uliniagiza kusitisha zoezi hilo ambapo nilitumia mtandao huo huo wa facebook kutangaza kusimama kwa zoezi hilo na kumwita ndugu Frank na kumzuia, naye akajuta sana kufanya kitu kwa maelekezo ya mtu badala ya chama. Mtakubaliana nami kwamba jambo hili ni hatari kwa mustakabali wa chama. Chetu na katibu wa mkoa ni shahidi kwamba imeanza kuwa ngumu kukusanya michango kwa wanachama wetu wengi wakihoji pesa wanazochangia chama kupitia kwa Lema zimetumikaje. 
  1. Kuuza vifaa vya chama kinyume na utaratibu

Wakati wa uchaguzi mdogo kata ya Daraja mbili, Mama Thea Mwase alikuwa anauza kadi kwenye mikutano ya hadhara ambazo alisema amepewa na Leman a kwamba baada ya mauzo anamplelekea hela yote Lema na yeye kupata commission. Hali hii ni kinyume cha taratibu za chama maana kadi za chama sio mradi binafsi na ni kinyume na azimio la Baraza kuu la chama katika kikao chake cha tarehe 29 Aprili 2012, kikao ambacho Bwana Lema alihudhuria. Hii pia inagusa kosa la kutumia mali za chama kwa maslahi binafsi kwa kuwa fedha hizo hajawahi kuzikabidhi kwenye chama bali huzitumia kwa mambo yake. 


  1. KUUNDA MAKUNDI NA KUENDESHA UASI DHIDI YA UONGOZI HALALI

Waheshimiwa viongozi, Lema ameunda kundi lake ambalo linapanga mkakati wa kuwapindua Viongozi wa Wilaya waliopo sasa hivi. Kundi hilo lina wajumbe wafuatao 

1. Calist Lazaro (Mwanachama) 2. Anorld Kamnde (Mwanachama) 3. Noel Ole Varoya (kaimu Mwenyekiti Bavicha (w) 4. Exaud Mamuya (Mwanachama) 5. Derick Magoma (Mwanachama) 6. Gabriel Lukas (Mwenyekiti kata ya Lemara) 7. Na huenda wengine ambao sijawajua 

Awali mkakati wao ulikuwa ni kutumia mkutano mkuu wa Wilaya kunipindua. Baadaye wakaja kugundua kwamba viongozi wengi wa kata wanaounda mkutano mkuu wa wilaya hawatakubaliana na mipango yao. Sasa kundi hili limepanga mkakati mpya ambao ni kufanya uchaguzi kwenye matawi na kuweka watu wao ili kwenye kata wawe wa kwao na baadae kwenye Wilaya. Kwa kuzingatia kwamba kuna waraka wa kamati kuu unaozuia chaguzi hizo za matawi na kata, kundi hili limeamua kuendesha mikutano ya hadhara minane mfululizo kwenye kata mbalimbali za Jiji la Arusha ili kujustify kwamba M4C imepita na kwa hiyo inawaruhusu wao kufanya chaguzi za matawi. Hadi sasa wanaendelea kurecruit watu wa kuingia kwenye timu yao kwa ajili ya kuzunguka kata zote. Vikao vingi hufanyika katika hotel ya Olduvai inn iliyopo jirani na East Africa Hotel ambapo ni ofisi ya Calist lazaro na mara nyingine nyumbani kwa Lema Njiro. Tabia hii ya makundi ilianza kabla ya uchaguzi wa Daraja mbili ambapo Lema alianza kutoa kauli ambazo zilionyesha kuwa ana mgombea wake. Kauli hizi alizitoa kwenye mkutano wa hadhara Kilombero. Hali hii ilisababisha makundi ambayo hatimaye yalitaka kuleta mgogoro kwenye chama. Baada ya hali kuwa mbaya alinipakazia kuwa mimi ndio nahamasisha wanachama jambo ambalo halina ukweli wowote. Hivi ninavyowasilisha mashtaka haya, kule Sombetini kuna kundi linalotaka kuondoa uongozi wa kata ili lipate nafasi ya udiwani, kundi ambalo mwasisi wake ni Ndugu Lema. Kila ninapomuuliza kutaka maelezo yake dhidi ya tabia yake ya kuvuruga chama, hunijibu kwamba yeye ni mjumbe wa kamati kuu na mimi sina mamlaka ya kumhoji. Daima Lema hataki kufuata mchakato wa wazi na wa kidemokrasia ambao utaleta mshikamano kwenye chama bali ni ujanja ujanja usio na msingi.

Ni katika vikao hivi na watu wake na wakati mwingine anapoonana na viongozi na wanachama wengine ambao anataka wamuunge mkono, amekuwa akipandikiza uchonganishi ndani ya chama, kutoa tuhuma na kashfa kwa uongozi na kupalilia migogoro kinyume na kanuni za chama. Lema: 

¨ Haheshimu viongozi wa wilaya na mkoa anamoishi isipokuwa tu pale wanapoonekana kukubaliana na kile anachokitaka yeye 


¨ Hachagui maneno ya kumwambia mtu gani wakati gani wala hafikirii madhara ya akisemacho. Kiongozi wa mkoa ama wilaya ama kata ama ngazi yeyote ya kuanzia mkoa kurudi chini akionekana kupingana na matakwa ya Lema mara moja atapachikwa ana hila dhidi ya Lema na hatakosa matusi kama alivyonitukana mwenyekiti wa Wilaya mjinga, mpumbavu, mshenzi, mwenye hila. Pia atambatiza kuwa ni mamluki wa ccm au usalama wa taifa au anatumiwa na mkuu wa mkoa 


¨ Lema anatumia vibaya ujumbe wa kamati kuu. Kwa Lema kuwa mjumbe wa kamati kuu kunamfanya awe kiongozi mkuu wa mkoa mzima anaoishi wa Arusha na kwa hiyo kuanzia mwenyekiti wa mkoa mpaka chini anawachukulia kama wako chini yake na yeye ndiye mwenye maamuzi ya mwisho kwenye mkoa 


¨ Lema kaja sasa na mbinu mpya ya kuwaspot baadhi ya viongozi waliopo kwenye mkoa na wilaya ambao anaona kabisa hataweza kuwatumia atakavyo, anawachafua kwa viongozi wengine na hata kwa wanachama,na kwenye mitandao ya kijamii hasa JF(jamii forums) ambako ana id mbili ninazozifahamu 


¨ Lema hivi sasa anaunda mtandao wake wa kuweka viongozi anaowataka yeye kwenye uchaguzi wa chama ngazi ya wilaya na mkoa, akipanga yupi lazima aondoke na yupi abaki. 


¨ Lema amefanya chama hivi sasa ngazi ya wilaya kiwe kina pro-Lema wengi na anti-Lema wa kutosha na hii si afya kwa chama 
Kwa kifupi, Lema anataka kuongoza chama Arusha kwa remote, na aweke watu watakaowajibika kwake badala ya kwenye CHAMA. 


Matendo haya yanapingana na kanuni za chama kama zilivyonukuliwa hapa chini: 

"10.1 {viii} Kiongozi anatakiwa kuwa mkweli na muwazi wakati wote hususan katika vikao halali na aachane na vikundi vya majungu, wadanganyifu (rumour mongers). Ni mwiko kwa kiongozi kujihusisha na upotoshaji wa maamuzi halali vya vikao vya chama, {ix} Kiongozi asijihusishe au kushiriki na vikundi au vitendo vya kuchonganisha au kuzua migogoro ndani ya uongozi wa chama au wanachama wake, {x} kiongozi asitoe tuhuma zozote juu ya viongozi wenzake pasipo kupitia vikao halali na kuzingatia taratibu na ngazi zilizoelezwa kwenye kanuni za chama" 

  1. MATUSI NA UDHALILISHAJI DHIDI YANGU:

Mara baada ya uteuzi wa mgombea udiwani kata ya Daraja mbili, Lema alinipigia simu jioni kwenye saa kumi na moja tarehe 03 Octoba 2012, akanitukana matusi makubwa ya nguoni kwa Dakika 20, na kunitishia kwamba ameshaongea na Mwenyekiti wa Taifa na kuwa lazima wanijadili na kunifukuza uanachama kwa madai ambayo kimsingi ni uongo wa kiwango cha juu, kuwa mimi mwenyekiti wa Wilaya sina uwezo, nimejaa hila, ni mzushi, ni mbabe, mbaya zaidi haya matusi amekuwa akinitukana wakati akiwa na wanachama wa kawaida. Tarehe 24/11/2012 Lema alinipigia simu kwa namba 0764150747, majira ya saa tisa alasiri.hata hivyo sikuweza kupokea simu hiyo kwa kuwa nilikuwa kwenye kikao kata ya Terat kwa ajili ya kutafuta suluhu kwenye mgogoro wa uongozi wa kata, mgogoro ambao ameutengeneza yeye kwa kumtumia katibu wa kata kumwondoa madarakani mwenyekiti wa kata kinyume cha katiba kwa sababu ya chuki binafsi dhidi ya mwenyekiti huyo. Baada ya kutopokea simu yake, ndipo akanitumia ujumbe mfupi wa maneno usemao, "Sikiliza , nakupigia kwa kuwa unaitwa mkiti wa chama wilaya na si sababu nyingine . Hata hivyo kutokupokea simu ni upuuzi wala sio ujasiri na nguvu". kutoka namba 0764 150747 saa 16:25Baada ya dakika 40 akatuma ujumbe mwingine: "Watu wako wamerudi CCM". 0764 150 747 saa 17:05 

Waheshimiwa Viongozi, naomba kuwasilisha malalamiko yangu na kuliomba Baraza la Uongozi la Mkoa kuchukua hatua za kinidhamu kwa mujibu wa Katiba, Kanuni na Maadili ya chama. 

Ephata Nanyaro, 
MWENYEKITI WA CHAMA 
WILAYA YA ARUSHA MJINI.


--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.
 
 

0 comments:

Post a Comment