Sunday 7 October 2012

[wanabidii] TAMKO LA PAMOJA LA KONGAMANO LA KITAIFA LA KUZUNGUMZIA NAFASI YA ZANZIBAR KATIKA MJADALA WA KATIBA MPYA

TAMKO LA PAMOJA LA KONGAMANO LA KITAIFA LA KUZUNGUMZIA NAFASI YA ZANZIBAR KATIKA MJADALA WA KATIBA MPYA, UKUMBI WA SALAMA, HOTELI YA BWAWANI, TAREHE 06 OKTOBA, 2012

Sisi washiriki wa Kongamano la Kitaifa la Wazanzibari tuliloliitisha kuzungumzia Nafasi ya Zanzibar katika Mjadala wa Katiba Mpya leo hii Jumamosi, tarehe 06 Oktoba, 2012 katika Ukumbi wa Salama, Hoteli ya Bwawani, mjini Zanzibar tunatambua kwamba fursa iliyopo mbele yetu katika Mjadala huu wa Kitaifa ni fursa adhimu ambayo inapaswa kukumbatiwa na kila Mzanzibari Mzalendo katika kuamua Mustakbali wa Zanzibar na watu wake.

Katika kuikumbatia fursa hii, tunatambua, kuheshimu na kuthamini hatua iliyofikiwa ambapo Wazanzibari kutoka makundi na taasisi tofauti wameungana na kuja pamoja katika kusimamia na kuendesha harakati zenye lengo la kuirejesha Zanzibar yenye mamlaka kamili kitaifa na kimataifa itakayofuatiwa na mashirikiano ya Muungano wa Mkataba kati yake na Tanganyika.

Hata hivyo, tunaelewa pia kuwa zimekuwepo jitihada za makusudi za kujaribu kuuvunja umoja huu wa Wazanzibari kwa kutumia hoja dhaifu zenye lengo la kutuondoa katika mstari ili kuzima vuguvugu la Wazanzibari.

Hatua ya leo ya kuwa na wasemaji na washiriki kutoka makundi na taasisi tofauti ni kudhihirisha kwamba njama za kutugawa tutazishinda kwa njia za amani na za kidemokrasia.

Kutokana na hali hiyo, ndiyo leo hii tumeamua sisi Wazanzibari tunaotoka makundi na taasisi tofauti lakini tunaounganishwa na UZANZIBARi na imani yetu kwamba wakati umefika wa ZANZIBAR kurejesha mamlaka kamili kitaifa na kimataifa, kutoa tamko LIFUATALO.

KWAMBA umoja wetu ndiyo nguvu yetu na ngao yetu, hivyo tumeamua kuunganisha nguvu zetu katika kusimamia madai halali ya Wazanzibari na kwamba tunakataa njama zote za kutaka kutugawa ili kuendeleza mipango ya wasioitakia mema Zanzibar ya kutaka kuendelea kuidhibiti.

KWAMBA tutaendeleza harakati hizi za Wazanzibari kwa njia za amani na za kidemokrasia.
KWAMBA hatutositisha harakati zetu za amani na kidemokrasia hadi lengo la ZANZIBAR yenye mamlaka kamili kitaifa na kimataifa litimie, na kwamba juhudi zozote za kutaka kubadilisha matakwa ya Wazanzibari kwa kuwakisia na kuwakadiria cha kuwapa hazitokubalika. Tunachokisimamia ni HAKI yetu na si OMBI au fadhila kutoka kwa yoyote.

KWAMBA tuna imani na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye muundo wa Umoja wa Kitaifa chini ya Raisi Muheshimiwa Dk. Ali Mohammed Shein na pia tunaimani na viongozi wetu. Na tunaamini Serikali yetu na viongozi wetu hao ni wazalendo wa Zanzibar na kwamba ridhaa yao imetoka kwa wananchi wa Zanzibar. Hivyo basi, tunaamini na kuwategemea kuwa kama wanavyoendelea kutuahidi watasimamia na kutetea matakwa na maamuzi ya Wazanzibari walio wengi.

KWAMBA tunatoa wito kwa Jumuiya ya kimataifa kufuatilia kwa kina mchakato wa katiba mpya na kufuatilia matakwa ya Wazanzibari wanayoyatoa katika mijadala mbali mbali inayoendelea. Tunaitegemea jumuiya ya kimataifa hatimae iunge mkono matakwa ya Wazanzibari yanayotolewa kwa njia ya amani na kidemokrasia.


KWAMBA Zanzibar tunayotaka kuiona ni Zanzibar itakayojengwa chini ya misingi YA UHURU, USAWA, DEMOKRASIA, UVUMILIVU, HAKI ZA BINAADAMU, AMANI NA UJIRANI MWEMA, NA YENYE MAISHA YA NEEMA KWA WATU WAKE WOTE.


ZANZIBAR KWANZA

Limetolewa leo
Tarehe 06 oktoba 2012
ZANZIBAR.

--
Karibu Jukwaa la www.mwanabidii.com
Pata nafasi mpya za Kazi www.kazibongo.blogspot.com
Blogu ya Habari na Picha www.patahabari.blogspot.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
 
 

0 comments:

Post a Comment