Monday 1 August 2016

[wanabidii] Biashara ya kuku wa kienyeji inavyoweza kukuondolea umasikini.


Watu wengi wamekuwa wakifikiria kuhusu namna ya kujikwamua kutoka kwenye umasikini.Leo hii nitawaelezea kuhusu biashara ya kufuga kuku wa kienyeji ambavyo inaweza kukukwamua kutoka kwenye umasikini. Lengo kuu ni kuwawezesha watu kutengeneza ajira kwao binafsi na watu wengine.
Takwimu za uzalishaji (kutaga, kuangua na kukuza kuku)
Utafiti uliofanywa na Dr. John Bishop kwa msaada wa shirika la kitaifa la utafiti wa kilimo nchini Equador na Chuo kikuu cha Florida nchini Marekani, umeonyesha kuwa ; Kama kuku akitunzwa vizuri kutokana na mbinu bora za ufugaji, anaweza Kuongeza uwezo wa kutaga mayai kutoka mayai 10 hadi mayai 12 kwa mwezi. Kwa mfano ukiwa na kuku 12 na jogoo 1 waliolishwa kilo 1 ya nafaka kila siku unaweza kuuza dazani 10 za mayai kila mwezi ambayo ni sawa na mayai 4 kila siku.
Jee unapenda kutajirika kwa kufuga na kuuza kuku?
Angalia mchanganuo wa mahesabu mapato yako yatakuwa kama ifuatavyo, Kwa kipindi cha miaka 2. K wa mtaji wa Sh. 500,000/= kama una eneo la eka 1 na mabanda ya kutosha kiasi cha kuku 10,000. Ukianza kwa kufuga kuku 25 ( kuku 20 na jogoo 5) ambao utawanunua kwa Sh. 250,000.00. Hao kuku 20 wakianza kutaga vifaranga 10 kila mmoja wataangua vifaranga 200 watunze vizuri katika vifaranga hao tuchukulie majike yanaweza kuwa 150 ambao ndani ya miezi 6 au zaidi nao wataanza kutaga. Kipindi hicho utakuwa na kuku (200+ 25 =225.) Baada ya hiyo miezi 6 kuku watakaotaga ni 170 kila mmoja akipata vifaranga 10 mpaka mwisho wa mwaka utakuwa na kuku (1700+20+55=1775) ukiuza kuku 1,000 kwa bei ya Tshs. 10,000 utapata Tshs. 10,000,000/=. Mwaka wa 2 majike 775 yakiangua vifaranga 10 kila mmoja utakuwa na kuku 7,550 mwisho wa mwaka ukiuza kuku 3,000 kwa bei ya Tshs. 10,000 utapata Tshs. 30,000,000/= Hesabu hizi ni kwa makadirio ya chini sana kwani kama nilivyoelezea hapo juu kuku mmoja kama atatunzwa vizuri anaweza kuataga mayai kati ya 10 hadi 12 kwa mwezi.
.Kuku wa kienyeji wamekuwa wakifugwa kwa wingi vijijini kwa malengo ya kupata nyama na mayai kwa ajili ya familia husika na kwa ajili ya kupata pesa za kujikimu. Kuku na mayai ya kienyeji yana faida kubwa kiafya kutofautisha na kuku wakisasa ambao hukuzwa kwa kemikali. Idadiya kuku Tanzania inakadiriwa kuwa na jumla ya kuku Milioni 34 wanaofugwa na takribani 60.5% ya kaya zinazojishughulisha na kilimo. Hata hivyo uzalishaji wake umebaki kuwa duni kutokana na changamoto za wafugaji zifuatazo; Utunzaji duni , Udhibiti mdogo wa magonjwa, lishe duni, makazi duni, Uzaliano wa karibu, Teknolojia duni, Kukosekana kwa mtazamo/mwamko wa kibiashara.
Faida ya kufuga kuku wa kienyeji.
Ufugaji wa kuku wa kienyeji una manufaa mengi kwa mfano; Kuku hutumia eneo dogo kuliko wanyama wengine wa kufugwa, pia hutumia chakula kidogo hivyo ufugaji unaweza kuendeshwa bila kutumia mtaji mkubwa. Kuku wanaweza kupewa mabaki ya chakula pamoja na vyakula vya kujitafutia kama vile wadudu,mbegu na majani. Kazi za usimamizi wa kuku zinaweza kufanywa na mama na watoto. Kuku na mayai humpatia mfugaji chakula bora na kumuongezea mapato. Pia mfugaji ni kama mtu aliyewekeza fedha zake benki au kwenye kitegauchumi kingine ambapo kuku huweza kuongezeka kutokana na kuku kutaga na kuangua vifaranga kama faida inavoongezeka benki na kwenye vitegauchumi vingine. Mfugaji ni sawa na mtu aliyeweka akiba benki kwani akipata shida anaweza kuuza kuku na kulipa ada, mahari matibabu ya hospitali pamoja na shida zingine. Kuku wa kienyeji anasaidia kusafisha mazingira kwa kula wadudu na kuongeza rutuba kwa mbolea inayotokana na kinyesi cha kuku ambacho hakina kemikali. Mbolea hii ni nzuri sana na kama inazalishwa kwa wingi inaweza kuwa chanzo kingine cha mapato kwa mfugaji wa kuku. Kuna mjasiriamali ninayemjua anafuga kuku wengi anazo tani nyingi za mbolea hii na anauza mbolea ya mavi ya kuku kwa Sh. 600 kwa kiloba cha kilo 50. Kuku wa kienyeji ana uwezo mkubwa wa kuhimili magonjwa, hutaga mayai na kutunza vifaranga badala ya kutumia mashine. Kuku wa kienyeji anaweza kuishi nchi yoyote duniani bila kuathiriwa na hali ya hewa.
Aina za magonjwa ya kuku na jinsi ya kukinga magonjwa.
Wapatie chanjo kuku wako kwa afya bora. Wapatie kinga mara kwamara kila baada ya miezi 3. Magonjwa yafuatayo ndiyo huwa yanawashambulia kuku.
New castle
Dalili za ugonjwa huu ni kuku kushindwa kupumua, kukohoa na kutokwa na mate,kuwa na kinyesi cha rangi ya kijani, ugonjwa huu hauna dawa. Chanjo hutolewa machoni kwa njia ya matone.
Minyoo.
Dalili za mionyoo ni kuku kukosa hamu ya kula uzalishaji wa mayai kupungua. Ukiona dalili hizo waone wataalamu wa mifugo upate dawa.
Wadudu.
Utitiri husumbua kuku, kwa kuwasababisha kukosa usingizi,ngozi kuharibika,huathiri uzalishaji wa mayai. Ukiona dalili hizi wasiliana na wataalamu wa mifugo upate dawa.
Magonjwa ya mapafu.
Huathiri sehemu za kupitishia hewa na kuwa na sauti ya kukoroma. Hali hii hupunguza uzalishaji wa mayai na uzito wa kuku kupungua. Ukiona dalili hizi wasiliana na wataalamu wa mifugo upate dawa.
Mambo mengine unayopaswa kuyajua kama mfugaji wa kuku
Inapokuja katika ufugaji wa kuku wa kienyeji ,mbinu inayotumiwa kijijini ile kuku huachwa azurure katika boma bila uchungaji ama na uchungaji mdogo.Kuna matatizo mengi ambayo kuku hukutana nayo. Kuku halishwi vyema kwani hula masalio ya.chakula na mabaki mengine wanayoyapata. Vifaranga wadogo huachwa washindanie chakula na kuku wakubwa na huwa nyama rahisi kwa wanyama wanaowinda na kula nyama na husambaza magonjwa. Kuku hawapati maji ya kutosha na hawana mahali pa kujisetiri dhidi ya upepo na mvua ama kuwaweka salama dhidi ya wanyama wanaowinda na kula nyama bila kusahau wezi. kuku hutaga mayai ardhini na yanaweza kuharibiwa kwa urahisi na kuliwa na wanyama wengine. Sio kawaida kuku kupewa chanjo na matibabu dhidi ya magonjwa na vimelea. Matokeo ni kuku wengi huwa wagonjwa na hukua pole pole,hutaga mayai machache na nyama kidogo.
Ili kuhakikisha mapato mazuri kutoka kwa kuku wako,fanya yafuatayo:
Kuwapatia kuku mgao mzuri wa vyakula tofauti na maji safi.Kutemeana na kipindi cha mwaka,wataweza kujitafutia chakula kwa kukwaruza ardhi katika boma. Wapatie chakula cha ziada ili kuku waongeze uzani na kuku watage mayai mengi zaidi. Walishe vifaranga na chakula kilicho na protini kama mchwa ili wakue kwa haraka na wawe na afya. Wajengee kuku mahali penye giza na patulivu ambapo wanaweza kutaga mayai yao.Kuku huhitaji kujisikia wakiwa salama kutoka kwa wanyama wanaowinda na kula nyama na wapita njia. Kama kuku watasumbuliwa mara kwa mara watakuwa wakiviacha viota vyao na hii huathiri uanguaji wa mayai. Ikiwa nia yako ni utoaji wa mayai,ni vizuri kufuga kuku wa kike pekee.Jogoo mmoja anaweza kufugwa aangalie wanyama wanaowinda na kula nyama na kuwahudumia kuku.Wakati jogoo wa ziada wanapofikia umri wa kuuzwa,wanafaa kuuzwa,kuchinjwa ama kutolewa kama zawadi kuzuia jogoo kula chakula ambacho ni adimu na kupigana na kuwataabisha kuku. Ukubwa wa kundi unafaa kuafikiana na ukubwa wa nyumba au banda ,kiasi cha chakula unachoweza kununua na raslimali za chakula katika maeneo yanayokuzunguka. Usinunue kuku kutoka katika vyanzo ambavyo havijathibitiwa haswa vipindi milipuko ya magonjwa ni kawaida kwa sababu wanaweza kusambaza magonjwa kwa wengine. Toa chanjo mara kwa mara kulingana na ushauri wa watoaji chanjo na madaktari wa wanyama wa nyumbani. Vifaranga wachanga wanapaswa kuchanjwa dhidi ya magonjwa ya kawaida ya kuambukizana wakifika umri wa wiki 2-3.
Ikiwa kuku watataabika kutoka kwa ugonjwa sugu unapaswa:
• Kuita daktari wa wanyama
• Kumwtenga kutoka kwa wengine
• kuku anafaa kuuliwa mara moja kwa kutegemea jinsi ugonjwa ulivyo mzito na
• Anafaa kuchomwa ama kuzikwa katika kina kirefu ili kuzuia mbwa na wanyama wengine kuwachimba na kusambaza ugonjwa.
Angalia ni kuku gani wana dalili za kutaka kuangua mara moja kwa mwezi na uwapatie matunzo ya ziada
CHARLES NAZI
Mwandishi wa makala hii ni Mkurugenzi wa Kampuni yaCPM Business Consultants kwa mawasiliano zaidi pigasimu namba 0755394701

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.

0 comments:

Post a Comment