Kwanza, kulingana na ibara ya 8 ya Katiba ya CCM, Kamati ya Siasa ya Halmashauri Kuu ya CCM ya Tawi ndio hufikiria na kutoa uamuzi wa mwisho kuhusu maombi ya uanachama.
Pili, kulingana na ibara ya 12 (1), baada ya mtu kukubali kuwa mwanachama inabidi atekeleze mambo yafuatayo, kabla ya kusajiliwa kwenye rejesta ya wanachama wa CCM: lazima atoe kiingilio cha uanachama; lazima alipe ada ya uanachama kila mwezi; na lazima atoe michango yoyote inayoamuliwa na viongozi wa CCM.
Tatu, kulingana na ibara ya 13(1) ya Katiba ya CCM (2010) uanachama wa mtu katika CCM unakwisha kutokana na sababu mojawapo kati ya sababu sita zifuatazo: kufariki, kujiuzulu, kuachishwa kwa mujibu wa Katiba, kufukuzwa kwa mujibu wa Katiba, kutotimiza masharti ya uanachama, au kujiunga na Chama kingine chochote cha siasa.
Na nne, kulingana na ibara ya 13(4) mwanachama aliyejiuzulu akitaka kuingia tena katika CCM ataomba upya kwa kufuata utaratibu wa kuomba uanachama kwa mujibu wa Katiba ya CCM.
Kwa kuzingatia vifungu hivi vinne vya katiba ya CCM (2010), mambo kadhaa yanafuata kimantiki.
Kwanza, ni wazi kuwa ibara hizi zinawakataza viongozi watendaji katika CCM kupokea kiingilio cha uanachama au ada ya uanachama kutoka kwa mtu ambaye ni mwanachama wa Chama kingine chochote cha siasa mbali na CCM. Yaani, kiongozi wa CCM anayepokea kiingilio cha uanachama au ada ya uanachama kutoka kwa mtu ambaye sio mwanachama wa CCM anakuwa ni kiongozi mwenye asiyefikiri sawasawa.
Na pili, kwa kuzingatia vifungu hivi vinne vya katiba ya CCM, ni wazi kuwa, mwanachama wa CCM ambaye anathibitika kuwa, baada ya kujiunga na CCM, ameamua kuwa mwanachama wa Chama kingine chochote cha siasa mbali na CCM, anapaswa ama kuachishwa kwa mujibu wa Katiba au kufukuzwa kwa mujibu wa Katiba ya CCM.
Hii maana yake ni kwamba, kiongozi wa CCM anayefahamu kuwa kuna mwanachama wa CCM ambaye amefanikiwa kuwa Katibu Mkuu au mbunge kupitia chama kingine chochote cha siasa lakini akasita kusimamia mchakato wa mtu huyo kuachishwa kwa mujibu wa Katiba ya CCM au mtu huyo kufukuzwa kwa mujibu wa Katiba hiyo hiyo, anakuwa ni kiongozi asiyefikiri sawasawa. Anakuwa ameisahau katiba yake.
Kwa kuzingatia mahitimisho haya mawili muhimu, sasa tunaweza kutambua kwa kurejea kauli ya Nape dhidi ya Slaa kuwa na kadi ya CCM, yeye (Nape) ni kiongozi wa namna gani.
Nape Nnauye, Katibu Mwenezi na Itikadi (CCM), amesema na kuandika katika mitandao ya kijamii maneno yafuatayo:
"Katika matamshi yangu hakuna mahali nilipohusisha kuwa na kadi na uanachama wa mtu.....hivyo wanaojaribu kubwabwaja kuwa sijui Katiba ya CCM wanakurupuka kwa sababu ndogo sana… nilichosema (ni kuwa) Dk. Slaa na baadhi ya vigogo wa (CHADEMA) wana kadi za (uanachama wa) CCM na baadhi yao wanazilipia mpaka leo.
Sijazungumzia uanachama wao...najua kuwa kwa katiba ya CCM ukishakuwa mwanachama wa chama kingine uanachama wako CCM unakufa hapo hapo.
Kwa mujibu wa nukuu hii, Nape Nnauye amejenga hoja mbili tata ambazo nakusudia kuzipa muundo wa kimantiki na kisha kuzihakiki kwa lengo la kumpa somo. Hoja ya kwanza ambayo Nnauye ameijenga kwa njia ya mzunguko ni hii hapa:
"Kwa mujibu wa katiba ya CCM, kila mwanachama hai anapaswa kulipa kiingilio cha uanachama na ada ya uanachama; Dk. Slaa ambaye ni Katibu Mkuu wa CHADEMA na baadhi ya vigogo wenzake katika CHADEMA wana kadi za uanachama wa CCM na baadhi yao wanafanya malipo haya mpaka leo; Kwa hiyo wao ni wanachama hai wa CCM. Hata hivyo, haya matamshi yangu dhidi yao hayahusianishi kadi za CCM walizonazo kina Dk. Slaa na uanachama wao katika CCM."
Katika hoja yake hii, Nape Nnauye ananishangaza mambo mawili. Kwanza anajaribu kutuambia kuna wanaCCM ambao ni wanaCHADEMA pia. Lakini pili, anatuambia kwamba, yeye haijui katiba ya CCM. Nitaanza na hili la pili nikiwa nimefanya dhahania (assumption) kwamba, siku ile Nnauye anatoa kauli zake inawezekana, angalau kimantiki, kwamba Dk. Slaa na wenzake wanaotajwa naye tayari walikuwa wameamua kuchukua uanachama wa CCM lakini wakasitisha nia yao baadaye kidogo.
Katika mtazamo wake kuhusu katiba ya CCM, tatizo liko hivi: Nnauye amemwongelea Dk. Slaa pamoja na "vigogo wengine" wa CHADEMA katika sentensi yenye kiunganishi cha "na." Hivyo, anachokiongelea kitaalamu tunakiita "mazingira ya kitu hiki pamoja na kitu kile" (both/and scenario), ambapo kuna Dk. Slaa kwa upande mmoja na "vigogo wengine" wa CHADEMA kwa upande mwingine. Anasema kwamba wote wanazo kadi za CCM na baadhi yao wanazilipia mpaka sasa.
Ni wazi kuwa, Dk. Slaa kama Katibu Mkuu wa CHADEMA anayo kadi ya uanachama wa CHADEMA tangu alipohamia katika chama hiki karibu miaka 15 iliyopita. Kwa hiyo, kiunganishi cha "na" katika sentensi ya Nnauye kinamaanisha kuwa, baadhi ya wale "vigogo wengine" wa CHADEMA anaowataja wana kadi za CHADEMA pia.
Na maneno "baadhi yao wanalipia kadi" katika sentensi yake yanamaanisha kuwa ama Dk. Slaa au mmojawapo kati ya hao vigogo wengine wa CHADEMA waliotajwa analipia ada ya uanachama wa CCM. Huwezi kulipa ada ya uanachama wa CCM kama sio mwanachama wa CCM. Kwa hiyo, kwa kuzingatia ukweli huu, inafuata kimantiki kuwa kauli ya Nnauye kuwa "baadhi yao wanalipia kadi" za CCM inaongelea uanachama wa kina Dk. Slaa katika CCM.
Hivyo, ni kinyume cha kanuni za mantiki, kwa Nnauye kusema kwamba, matamshi yake haya "hayahusianishi kadi za CCM walizonazo kina Dk. Slaa na uanachama wao katika CCM." Huu ni usahaulifu.
Kuna hoja ya pili ambayo imesanifiwa na Nape Nnauye na ambayo inakoleza zaidi mtazamo wangu huu dhidi yake na wenzake. Katika nukuu yake hapo juu, kwa njia ya mzunguko, Nnauye pia amejenga hoja ifuatayo:
"Kwa mujibu wa katiba ya CCM, kila mwanachama hai anapaswa kulipa kiingilio cha uanachama na ada ya uanachama; Dk. Slaa ambaye ni Katibu Mkuu wa CHADEMA na baadhi ya vigogo wenzake katika CHADEMA wana kadi za uanachama wa CCM na wanafanya malipo haya mpaka leo; Kwa hiyo, viongozi watendaji wa CCM wanapokea kiingilio cha uanachama na ada ya uanachama kutoka kwa wanachama wa vyama vingine vya siasa! Hii maana yake ni kwamba, baadhi ya wanachama wa vyama vingine vya siasa ni wanachama wa CCM pia, jambo ambalo ni kinyume cha katiba ya CCM."
Huyo ndiye Nape Nnauye katika rangi zake halisi! Ameivua nguo CCM! Alichofanya hapa ni kulitangazia taifa na dunia nzima kwamba, CCM inaendeshwa nje ya utaratibu wa kikatiba!
Ni hivi: Kama anachokisema ni kweli, basi jambo hili ilipaswa kuwa sababu ya kutosha ya vikao husika ndani ya CCM kuanzisha mchakato wa kikatiba ili kufanikisha kuachishwa au kufukuzwa kwa kina Dk. Slaa kutoka CCM. Vinginevyo, vikao vya juu vinapaswa kuisambaratisha sekretarieti ya CCM ya sasa kwa kuvunja katiba ya CCM!
Nape Nnauye na sekretarieti yake lazima washughulikiwe kwa sababu wao wamethibitisha kwamba ni viongozi wenye kusumbuliwa na tatizo la kutokujipanga na kusimamia katiba ya chama chao.
Na kwa kuhitimisha basi, nataka niseme kwamba, Nape Nnauye, Katibu Mwenezi wa CCM, pamoja na sekretarieti yake yote inayofanya madudu haya aliyoyatangaza kwa dunia nzima tayari wamepoteza sifa ya kubaki katika ofisi wanazoziongoza.
Tutawashangaa sana kina Jakaya Kikwete (Mwenyekiti CCM), kama wataendelea kuwakumbatia viongozi hawa wanaosumbuliwa na tatizo la usahaulifu wa kiwango hiki kuhusu katiba ya chama chao, wakati ndani ya chama chao kuna watu wenye umakini mkubwa wa kushika nafasi hizi za uongozi.
Ni Makala ya Deusdedit Jovin kwenye gazeti la raia mwema.
*TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI, WANACHADEMA NA UMMA WA WATANZANIA JUU YA
MWENENDO WA UNDUMILAKUWILI WA BWANA WILBROD PETER SLAA KATIBU MKUU WA
CHADEMA TAIFA.*
Ndugu wanahabari rangi nyeupe katika bendera chama changu ninachokipenda
(CHADEMA) chama changu ninachokipenda inasimamia ukweli na uwazi. Rangi
hiyo inawataka wanachadema wote kuwa wazi katika kulinda, kusimamia
falsafa, itikadi na sera za chama chetu.
Nimehuzunishwa sana ka kukatishwa tama na kitendo cha undimilakuwili na
umamluki wa Katibu Mkuu Bwana Slaa kwa kitendo chake cha kuendelea kumiliki
kadi ya Chama cha Mapinduzi wakati akitambua kuwa yeye ni Kiongozu
anyeongoza harakati za chama Kikuu cha Upinzani hivyo kutakiwa kuwa mfano
bora wa kuigwa kwa kuonyesha mwenendo bora kwa kuishi maisha anayohubiri.
Katiba ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) sura ya tano ibara ya
kwanza ndogo ya 5.1.6 kinachosema "Mwanachama wa CHADEMA asiwe mwanachama
wa chama kingine cha siasa baada ya kujiunga na CHADEMA" Akitambua kadi
ndicho chombo kikuu kinachomtambulisha mwanachama ndani ya chama hivyo,
kitendo cha kuendelea kumiliki na kulipia kadi *Chama cha
Mapinduzi*kimedhihirisha kuwa yeye ni mbwa mwitu aliyejivika ngozi ya
kondoo ndani ya
upinzani.
Bwana Slaa amekuwa akiaminisha Umma kuwa yeye ni Kiongozi mzalendo safi
huku akiendelea kuwatuhumu baadhi ya wanachama na viongozi wenzie kuwa ni
mapandikizi,Hivyo kitendo hicho cha yeye kumiliki na kulipia ya CCM
imeonyesha kuwa yuko CHADEMA kwa kazi maalum ya kuhujumu harakati za
Ukombozi hivyo hana na amepoteza sifa ya kuwa Kiongozi wa Upinzani. Kwa
mujibu wa Katiba ya CHADEMA ibara ya tano, BWANA WILBROAD PETER SLAA NI
PANDIKIZI kutokana na sababu zifuatazo, ambazo nimejiridhisha nazo bila
chembe ya shaka yoyote hivyo tunamuomba apishe uchunguzi dhidi yake ili
tukiona dhamira njema tuendeleze harakati za Ukombozi yeye amepoteza sifa,
kwa kitendo cha kuwa na Kadi ya chama ambacho kimetesa Watanzania na
kuwanyanyasa lakini yeye bila aibu kukusanya kadi za wananchi wanaojiunga
na CHADEMA kuzichoma moto na huku yeye akiwa amebaki na yake kibindoni hii
imepelekea yeye kufanya kazi na umamluki na kukivuruga Chama kama
ifuatavyo:-
Amekuwa akitumika kugawa Mabaraza ya chama kwa kuidhinisha kumlipa mshahara
Mwenyekiti wa BAVICHA Taifa Ndugu JOHN HECHE kinyume cha Katiba na mwongozo
wa baraza la Chama ilihali Viongozi wengine wa Kitaifa wa mabaraza hata
wale wa Mikoani na Wilayani hawalipwi chochote wakati wao ndio
wanaohangaika kukijenga Chama.
Hii inaonyesha Bwana Slaa analipa fadhila kwa mwenyekiti huyo ambaye
maamuzi yote ya baraza huamiliwa na Bwana Slaa, Mfano huu wakulipana
fadhila anaoufanya Bwana Slaa ni mfumo wa CCM ambako Slaa ni mwanachama na
baada ya kukiri kwamba ni kweli anamiliki Kadi ya CCM hadi leo hii.
Bwana Slaa ni Kiongozi anyejihusisha na vikundi vya majungu jambo ambalo ni
kinyume na Katiba na kanuni ya Chama kwa kudhihirisha kwamba Bwana Slaa ni
mamluki ndani ya CHADEMA aliyekuja kutimiza kazi maalumu amekuwa akichochea
mgogoro na kuchukua maamuzi ya kuwafukuza baadhi ya vingozi ambao
wamekiongoza chama kwa muda mrefu.
Bwana Slaa alifukuza viongozi wa chama Geita. Alifukuza madiwani Arusha.
Hapa Mwanza alishinikiza kufukuzwa kwa madiwani wawili *CHAGULANI NA
MATATA*bila kuzingatia falsafa ya Chama kuamini katika nguvu ya umma
kwamba
wananchi ambao ndio wapiga kura wenye maamuzi juu ya hao Madiwani
hawakushirikishwa katika kutoa maamuzi wakati wa kuwafukuza.
Bwana Slaa amesababisha madiwani watatu kufukuzwa hapa Mwanza kwakuwakataza
wasihudhurie vikao vya Halmashauri. Hivyo kwasababu kupoteza kata tatu (3)
ambazo ni Ilemela, Nyamanoro na Kirumba. Kwa madai kwamba hawamtambui *Meya
MATATA.*
Pia Bwana Slaa amekuwa akivunja uongozi wa chama bila kuzingatia Katiba ya
Chama kama Geita, Nyamagana, mvomero Morogoro Lindi na Mtwara bila kufata
Katiba kama inavyoeleza Ibara ya 6.3 (b) mamlaka ya nidhamu na uwajibikaji,
"kwamba kingozi aliyeteuliwa na vikao vya uongozi ataweza kusimamishwa au
kuachishwa Uongozi na Kikao kilichomteuwa"Lakini yeye amekuwa akifukuza na
kuvunja Uongozi katika sehemu mbalimbali za nchi bila kuzingaita misingi ya
Katiba, Anaongoza Chama kwa Mfumo wa Hailakia kwamba atakalosema yeye ndio
sheria na linalotakiwa kufuatwa na haitakiwi kuhoji. Slaa amekuwa
akiwafukuza na kuwaita kwa kuwatukana mamluki Vingozi ambao wamejenga Chama
kwa muda mrefu bila hata ruzuku leo hii chama kinapata ruzuku ya zaidi ya
Milioni 200 wanaonekana hawafai licha ya kutopelekewa ruzuku majimboni mwao.
Vilele Bwana Slaa amekuwa akilazimisha Viongozi wa Chama Mikoani kumpokea
anaedaiwa kuwa mchumb wake bibi JOSEPHINE MSHUMBISI kama Kiongozi wa chama
Taifa,mchumba wake amekuwa chanzo pia cha migogoro ndani ya chama kwani
amekuwa akipeleka watu majimboni na kuagiza viongozi wa Chama wamtambue
kama mgombea wa ubunge mwaka 2015, Pia amekuwa akitumia rasiliamali za
chama vibaya katika ziara yake.
Amekuwa akichangisha michango kwa kisingizio cha M4C ( vuguvugu la
mabadiliko) Huku pesa hizo akizitumia kwa ajili ya taasisi yake yake
binafsi iitwayo JUKWAA LA WANAWAKE kwa kifupi Josephine Mshumbusi
haifahamiki kama ni mwanachama wa CHADEMA au La:- Hivyo Bwana Slaa hatuna
imani nae kwani vitendo hivyo vyote vinatishia usalama wa Chama.
Jambo lingine la kusikitisha kwa wana – nyamagana na Mwanza nzima kwa
ujumla bwana Slaa amemteua Ezekiel wenje mbunge wa Nyamagana kuwa
mkurugenzi wa mambo ya nje makao makuu ya chama Dar es salaam hivyo
wananchi wa Nyamagana hawana mbunge kwani kwa sasa anaishi Dar es salaam na
kufanya kazi huko. Sasa hivi wana- nyamagana hawana tena mbunge kwani yuko
Dar es salaam amekuwa mbunge wa makao Makuu.
Ndugu waandishi ,katika kudhihirisha kuwa Wenje sasa hivi sio mbunge wa
wanachi bali mbunge wa Makao Makuu, Ndugu Wenje haelewi suala lolote
linaloendelea jimboni kwake kwani ninyi wanahabari ni mashahidi alipotoa
tamko la Uongo mbele yenu akidai machinga wa Mwanza wamesema wanampa siku
14 Mkurugenzi wa Jiji awe amejiuzuru , jambo ambalo lilithibitisha kuwa ni
la uzushi kwani SHIUMA (Shirika la Umoja wa Wamachinga). Lilimjibu na
kumtaka afute kauli yake kwani hajazungumza wala kuwahi kuonana na
wamachinga aache kuwachonganisha na Serikali kwa manufaa yake binafsi kwani
hao wameendelea kuchapa kazi ili kujiletea maendeleo wakishirikiana bega
begani na Mstahiki Meya na madiwani wao.
Ndugu wanahabari katika hili bwana Slaa hawezi kukwepa lawama hivyo basi
kama ana uso wa aibu apishe kiti akae pembeni tujenge chama chetu.
*Ndugu wanahabari:*
Naamini mnakumbuka mwishoni mwa mwaka huu bwana Slaa alipokuwa anafanya
ziara ya kukagua uhai wa Chama Mkoa wa Dar es saalm na majimbo yake
alisikika akitekeleza na kuunga mkono mfumo kandamizi na unaofinya
Demokrasia na utumiaji mbovu rasimali za nchi hii kwakuwa na wakuu wa Mkoa
na Wilaya cha kustaajabisha na kushangaza bila aibu wala soni Bwana Slaa
aliwataka viongozi wa Ngazi mbalimbali katika Jimbo la Kigamboni (Chadema)
wawe tayari kupewa ukuu wa Wilaya na Mikoa Chadema itakapo kuchukua dola.
Kitendo cha bwana Slaa kuendeleza sera za CCM kama kuwepo kwa wakuu wa
Wilaya na Mikoa kinapingana moja kwa moja na sera na itikadi za CHADEMA.
Kauli tata kama hii inamuhalalisha bwana Slaa kutumikia mabwana wawlili
yaani CCM na CHADEMA ndio maana tunamtaka arudishe kadi ya Chadema na
aendelee na Chama chake cha CCM anachotekeleza sera na itikadi zake.
Ndugu Nadhani mnakumbuka tarehe 28 /10/2012 tulikuwa na uchaguzi mdogo wa
madiwani baada ya nafasi hizo kuachwa wazi kwa sababu mbalimbali. Katika
uchanguzi ule CHADEMA iliambulia viti 5 (vitano) kati ya viti 29. Lakini
baada ya kufanya uchunguzi wa kina kwa nini CHADEMA ilifanya vibaya katika
uchanguzi mpaka kupelekea kupata viti vichache kiasi hiki wakati CHADEMA
kwa sasa ni chama pendwa kwa Watanzania uchunguzi unaonyesha kwamba katika
uchaguzi ule wa madiwani Bwana Slaa ambae alizunguka katika kata zote
zilizokuwa zimeachwa wazi hakuwa na agenda ya kuhakikisha CHADEMA inashinda
bali alibeba agenda yake binafsi na chama chake pendwa CCM NDIO maana Kanda
ya ziwa CHADEMA tulishinda kwa asilimia 99 kwa sababu ya hujuma ya
undumilakuwili Bwana Slaa.
*Ndugu wanahabari:*
Vyanzo vya mapato katika Vyama vya Siasa ni ruzuku kutoka Serikalini,
michango mbalimbali kwa wadau, ununzi wa kadi za vyama kwa wanachama na
kulipia ada ya uanachama katika vyama vyao. Bwana Slaa anakichangia CCM ili
kiendelee kujiimarisha zaidi kwa kulipia ada ya uanachama . Kwa hio ujenzi
na uimarishaji wa CCM unasaidiwa na uwepo wa Bwana Slaa na michango yake
katika CCM.
*HITIMISHO:-*
Kutokana na mwenendo wa Bwana Slaa Wilbroad ninataka mwenyekiti wa Chama
Taifa achukue maamuzi sahihi ya kutuepusha na janga hili ndani ya Chama
maana ni bora uwe moto au baridi kuliko kuwa vugu vugu endapo akishindwa
tutaitisha maandamo nchi nzima maana Ni watanzania wazalendo wengi
walioumia, kifilisika, na hata kupoteza maisha wakipigania ukombozi wa nchi
hii, leo hii mamluki kama WILBROAD PETER SLAA hatuweai kukubali waturudishe
nyuma katika harakati za Ukombozi. Tunamtaka ajiuzuru haraka iwezekanavyo.
Hakuna kulala mpaka kieleweke.
*……………………………..*
*MIMI SALVATORY MAGAFU*
*KATIBU BAVICHA MKOA WA MWANZA.*
*nakala:wajumbe wote wa BAVICHA TAIFA*
Source: JF
--Jobs in Africa - www.wejobs.blogspot.com
nafasi mpya za Kazi www.kazibongo.blogspot.com
Habari na Picha www.patahabari.blogspot.com
DELL LATITUDE D 620 & D30
80 GB HardDisk ,CORE 2 DUO , 2.0 GHZ CPU ,1 GB RAM
DVD/CD - RW ,WINDOWS 7 /WINDOWS XP ,WIRELESS , BLUE TOOTH .
TSHS : 360,000 , 1 YEAR WARRANTY
CALL : 0786 806028
Free Delivery in Dar es salaam
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
0 comments:
Post a Comment