Tuesday 29 March 2016

[wanabidii] Serikali yaipuuza Marekani

WAKATI Bodi ya Shirika la Changamoto za Milenia (MCC) ikitangaza kuinyima Tanzania msaada wa Dola za Marekani 473 (zaidi ya Sh trilioni 1), Serikali imesema ilishajiandaa kuhusu hatua hizo na fedha hizo haikuzijumuisha katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha wa 2016/17.

MCC imezuia fedha hizo za maendeleo kutokana na hatua ya Tanzania kuitisha uchaguzi wa marudio ya Zanzibar pamoja na kutumika kwa Sheria ya Makosa ya Mitandao. Chini ya Mpango wa Uwekezaji wa MCC–2, fedha hizo zilikuwa ziende katika kuboresha huduma za umeme, ikiwamo kusambaza umeme katika vijiji vingi zaidi nchini.

Kiasi cha asilimia 46 ya Watanzania kwa sasa wanapata umeme kutoka asilimia 10 ya mwaka 2005 na sehemu kubwa ya asilimia hiyo ilitokana na msaada wa MCC-1. Fedha hizo zilikuwa ni awamu ya pili ya msaada kutoka MCC na tayari katika awamu ya kwanza, Tanzania ilipokea Dola za Marekani milioni 698 ambazo zilitumika kwa ajili ya ujenzi wa barabara za Tunduma- Sumbawanga, Tanga-Horohoro na Namtumbo-Songea-Mbinga.

Fedha hizo zilitumika kujenga upya mfumo wa huduma za maji kwa ajili ya miji ya Dar es Salaam na Morogoro na zilitumika kusambaza umeme katika vijiji vya mikoa 10 ya Tanzania Bara, zilitumika kutandaza njia ya pili ya kusafirisha umeme chini ya Bahari ya Hindi kati ya Bara na Tanzania Visiwani na pia zilitumika kujenga barabara zote kuu za Kisiwa cha Pemba na baadhi ya barabara za Unguja kwa kiwango cha lami.

Kauli ya Waziri wa Fedha Akizungumzia na gazeti hili jana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Phillip Mpango alisema tangu Desemba mwaka jana walishasoma alama za nyakati na hivyo kuamua kutozijumuisha fedha za MCC-2 katika maandalizi ya Bajeti ya Serikali yanayoendelea kwa mwaka ujao wa fedha.

"Tulisoma kwenye mitandao matamshi ya viongozi wa Mfuko huo ndio maana tukaamua kutozijumuisha fedha za MCC kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha, hivyo Watanzania wasiwe na wasiwasi juu ya kusitishwa kwa msaada huo," alisema Dk Mpango.

Hata hivyo, alisema Serikali itatoa tamko rasmi baada ya kupata barua kutoka MCC ikiwaeleza wamesimamisha msaada huo hadi lini na nini Tanzania inatakiwa kufanya ili kupata msaada huo. "Sisi tukipata hiyo barua tutaitafakari na tutawajibu," aliongeza waziri. Alisema Serikali bado inaamini uhusiano wa Tanzania na Marekani ni mzuri na wa muda mrefu hivyo huko mbele kutakuwepo na maelewano na fedha hizo zitatolewa.

"Sisi sio nchi ya kwanza kusimamishiwa msaada huo, Malawi waliwahi kunyimwa lakini baadaye walipewa, na mimi bado naamini tutaelewana huko mbele ya safari," alibainisha. Dk Mpango pia alitoa mwito kwa Watanzania kuiunga mkono Serikali inapokusanya maduhuli kutoka vyanzo visivyo vya kodi na wahakikishe wanalipa kodi inayostahili ili nchi iondokane na utegemezi wa wahisani.

"Hili liwe fundisho kwetu kwamba nchi itapiga maendeleo kwa kutegemea vyanzo vya ndani, hatuwezi kuwa tegemezi miaka yote ni lazima ifike mahali tusimame kwa miguu yetu na tutafanikiwa tu iwapo tutalipa kodi stahiki," alisema Dk Mpango.

Uamuzi wa MCC Desemba 2015, Bodi ya Wakurugenzi ya MCC iliahirisha upigaji kura ya kuichagua tena Tanzania kufuzu vigezo vya kupata mkataba wa mpya wa MCC kutokana na kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi Zanzibar na kusisitizia haja ya kukamilishwa haraka, kwa haki na kwa amani kwa mchakato wa uchaguzi.

Aidha, Bodi ilihitaji kupata uthibitisho kutoka kwa Serikali ya Tanzania kwamba Sheria ya Makosa ya Mitandao isingetumika kukwaza uhuru wa kujieleza na kujumuika, hususan kuhusu matumizi ya sheria hiyo kuwakamata watu kadhaa wakati wa uchaguzi. Wasiwasi huu ulirejelewa mara kadhaa, ikiwa ni pamoja na katika tamko lililotolewa na Balozi Mark Childress.

Mojawapo kati ya vigezo vya msingi kabisa ambavyo MCC hutumia kuingia ubia na nchi yoyote, ni dhamira ya dhati ya nchi hiyo kuimarisha demokrasia na kuendesha chaguzi zilizo huru na za haki.

Chaguzi visiwani Zanzibar na matumizi ya Sheria ya Mtandao yanakwenda kinyume kabisa na dhamira hii, imedai Marekani. "Kwa sababu hiyo, wakati ambapo Marekani na Tanzania wanaendelea kuchangia vipaumbele vingi, Bodi ya Wakurugenzi ya MCC imeona kwamba Serikali ya Tanzania imekuwa ikichukua hatua zisizoshabihiana na vigezo vya kupata sifa ya kuingia ubia na MCC. Hivyo basi, Bodi ilipiga kura kusitisha ubia wake na Serikali ya Tanzania.

Kwa hali hiyo, MCC inasimamisha shughuli zote zinazohusiana na maandalizi ya mkataba wa pili na Tanzania," ilieleza. Balozi wa Marekani anena Katika tamko lake, Balozi wa Marekani nchini Mark Childress alisema, "Ninaunga mkono kikamilifu uamuzi huo wa Bodi wa kusitisha maandalizi ya mkataba wa pili. Marekani na Tanzania tumekuwa na uhusiano wa muda mrefu na wa kina katika sekta nyingi.

"Tukiwa mbia mkubwa zaidi wa maendeleo kwa Tanzania, Marekani itaendelea kufanya kazi pamoja na Tanzania katika kuboresha afya na elimu, kukuza uchumi na kuimarisha usalama," alisema Balozi Childress. Maoni ya wachumi Mkurugenzi wa Asasi ya Utafiti wa Kupunguza Umaskini (REPOA), Profesa Samuel Wangwe alisema athari ya msaada wa MCC ni ndogo kwa uchumi wa nchi kwa kuwa nusu ya fedha hizo zingerudi Marekani kutokana na mfumo wa masharti hayo.

Alisema dawa ya kujitegemea ni kama ile aliyoitoa Rais John Magufuli kutumia rasilimali za ndani kuendeshea shughuli za maendeleo badala ya kutegemea misaada kutoka nje. Profesa Wangwe alihoji kama suala ni kuminya demokrasia, vitendo ambavyo Marekani imefanya Irak na Libya ndio kielelezo cha demokrasia?

Alisema kuna haja kubwa ya kuwa na chombo cha umoja wa kimataifa kifafanue demokrasia gani inakubalika ulimwengune, lakini sio kwa maana inayotaka Marekani. Naye Mtaalamu wa Uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Haji Semboja alisema Marekani haina rafiki katika nchi maskini na haina utamaduni wa kuzisaidia nchi maskini isipokuwa inasaidia pale inapokuwa na ajenda zake na pale inapotokea wanabadili ajenda zao lazima watoe sababu ya kusitisha msaada.

"Misaada ya kimarekani ni ya kipuuzi na hata watu wenye akili hawawezi kuupigia bajeti kwa sababu wakati wowote taifa hilo linaweza kutoa sababu za kipuuzi kukunyima msaada ambao imekuahidi na hiki ndicho kilichotokea kwani suala la Zanzibar halihusiani na msaada huo," alisema Dk Semboja. Alisema kisingizio cha Zanzibar na sheria ya mitandao kilichotumiwa na Marekani havina maana na hiyo inatokana na taifa hilo kutokuwa na historia ya kuzisaidia nchi maskini kwa sababu.

Alisema msaada wa MCC ulitokana na urafiki uliokuwepo kati Rais George Bush na Rais Kikwete na sio kati ya Serikali ya Tanzania na Marekani. "Serikali haikupaswa kuweka fedha za msaada wa Marekani kwenye bajeti, wenzetu wa Kenya walishafanya hivyo kwa sababu ya ubabaishaji wa Marekani, lakini sisi kwa kuwa ni masikini wa akili tunaweka bajeti kwa kutegemea mfuko wa mtu mwingine na madhara yake ndo haya," alisema Dk Semboja.

Naye Mkuu wa Shule ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Ulingeta Mbamba alisema ni kweli kufutwa kwa msaada huo kutakuwa na athari kwa uchumi ila akaeleza kuwa kama nchi ni lazima ijenge misingi ya kujitegemea. "Sijalisoma hilo tamko lao, ila najua hizo fedha ilikuwa ziende kwenye umeme, hili liwe funzo kwetu kwamba msaada sio suluhu ya maendeleo ya nchi yetu, kujitegemea ni kuzuri zaidi," alisema Profesa Mbamba.

Kigeugeu cha MCC Septemba 26, 2015, Rais mstaafu Jakaya Kikwete alihakikishiwa na Mtendaji Mkuu wa MCC, Dana Hyde katika mkutano uliofanyika katika Hoteli ya JW Marriot Essex House, New York, na kuhudhuriwa na watumishi waandamizi wa MCC akiwamo Kamran Khan, Makamu wa Rais wa Operesheni za MCC.

"Hongera Rais kwa sababu nchi yako, Tanzania imetimiza masharti yote ya kupata fedha nyingine chini ya mpango wa MCC - 2, ikiwa ni pamoja na uongozi wa MCC kuridhika kuwa Tanzania inachukua hatua za dhati kupambana na rushwa," alisema Hyde wakati huo akimueleza Rais Kikwete.

Mwenyekiti wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry imeafiki kuhusu kipengele pekee kilichokuwa kimebakia katika masharti ya kupata fedha za MMC kuwa ni kweli Tanzania inakabiliana ipasavyo na rushwa na kuchukua hatua stahiki kukabiliana na janga hilo la rushwa.

0 comments:

Post a Comment