Wednesday 30 September 2015

Re: [wanabidii] Mbeya na aibu ya vurugu za kisiasa

Mbona hajazungumzia kitendo cha polisi kupiga mabomu ya machozi kwa wananchi wa Tanga waliotoka kwenye mkutano wa Lowassa?

Sent from my BlackBerry® smartphone provided by Airtel Tanzania.

From: "'lang'itomoni lokomoi' via Wanabidii" <wanabidii@googlegroups.com>
Sender: wanabidii@googlegroups.com
Date: Wed, 30 Sep 2015 19:29:50 +0000 (UTC)
To: ELISA MUHINGO' via Wanabidii<wanabidii@googlegroups.com>
ReplyTo: wanabidii@googlegroups.com
Subject: [wanabidii] Mbeya na aibu ya vurugu za kisiasa

Mbeya na aibu ya vurugu za kisiasa

FUJO zilizofanywa na kikundi cha vijana pale Uyole, jijini Mbeya mwishoni mwa juma, zimewachanganya wakazi na wenyeji wa Mkoa wa Mbeya. Baadhi wakijiuliza kilichousibu mkoa wao, na kama ni jambo la kujivunia.

Kutokana na fujo hizo za Uyole, baadhi wameingiwa na hofu ya vitendo hivyo vya fujo na vurugu kugeuka kuwa utamaduni mpya wa mkoa huo, moja ya mikoa ya kimkakati katika siasa za nchi, hususani kwenye chaguzi.

Akiwa njiani kuelekea wilayani Mbarali kutoka Uwanja wa Ndege Songwe, mgombea wa nafasi ya urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, Jumapili iliyopita alisimamishwa na wananchi waliojikusanya katika maeneo mbalimbali yaliyopo kwenye barabara kuu ya Tanzania-Zambia, wakitaka awasalimie.

Hata hivyo, alipofika eneo la Uyole, ikiwa ni baada ya kupita na kusalimiana na wananchi katika maeneo ya Mbalizi, Iyunga, Mwanjelwa na Mamajoni, kilijitokeza kikundi kidogo cha vijana miongoni mwa wananchi waliokusanyika na kufanya fujo kwa kuzomea, huku wakimwonyesha vidole viwili, alama inayotumiwa na Chadema, pamoja na kuimba Lowassa, Lowassa, Lowassa.

Dk Magufuli hakuonyesha hasira bali aliwapozesha kwa kuwasalimia na kuwaomba kumpigia kura, akisema yeye atakuwa Rais wa Watanzania wote, na kuibuka na kauli ya "Mbeya for Change."
Watofautiana kuhusu chanzo cha fujo

Pamoja na kutofurahishwa na vurugu za kisiasa ambazo zimekuwa zikijitokeza mkoani humo, ikiwamo zomea zomea ya viongozi, kuna kutofautiana kimtazamo kuhusu kiini cha vurugu hizo mkoani humo.

Wakati baadhi wakiwanyoshea kidole viongozi kuwa chanzo cha hasira ya vijana mkoani humo dhidi yao, wengine wanaamini kuwa ni vurugu zenye kuratibiwa kwa maslahi ya kisiasa.

Hoja ya vurugu hizo kuandaliwa na kuratibiwa na kundi lenye maslahi ya kisiasa, inajengwa kutokana na mazingira zilivyotokea, kwamba vijana hao walishindwa kutimiza lengo lao hilo maeneo mengine aliyosimamishwa Magufuli, ikiwamo Mwanjelwa, ambako ndipo penye kuaminika kuwa chanzo cha vurugu za kisiasa zinazotokea jijini Mbeya.

Kundi hili la pili linaziangalia vurugu hizo kama taswira mbaya kwa mkoa huo, hawazionei fahari wakiamini kuwa zinawadhalilisha wananchi wa mkoa huo, wanaviona kuwa ni vitendo vya kihuni, vyenye kujenga taswira chafu kwao.

"Ule sio ustaarabu, walichokifanya wale vijana sio cha kistaarabu, kuna maisha baada ya uchaguzi," anasema mwandishi mwandamizi nchini, Lauden Mwambona.
Wananchi hao wanaziangalia vurugu hizo kwa jicho la aina ya siasa za chuki zenye kuudhalilisha mkoa, kiasi cha kuonekana kuwa mkoa wa wahuni.

Huko nyuma baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa mkoani humo waliibuka na kauli ya "Mbeya kwanza vyama vya siasa baadaye," kauli ambayo baadaye viongozi wa siasa kitaifa walichukua wakisema, "Tanzania kwanza vyama baadaye."

Mwenyekiti wa APPT Maendeleo, Godfrey Mwandulusya, anakielezea kitendo cha vikundi vya wanachama vijana wa vyama vya siasa mkoani humo kuendesha vurugu dhidi ya vyama vyama vingine vinadhihirisha udhaifu mkubwa ulipo kwenye vyama vyao.

Hata hivyo, Mwandulusya anabainisha kuwa vitendo hivyo vimemjenga zaidi mgombea wa CCM, Dk Magufuli, mkoani humo badala ya kumdhoofisha kama lilivyo lengo la wapinzani wao.

"Kwa upande mwingine, vitendo hivyo vimeonyesha ni jinsi gani Magufuli anafaa kuwa Rais, amefanya kile ambacho wengi wameshindwa kwa kutumia salamu ile ile wanayomkejeli nayo, kuwasalimia na kuwaomba kura," anasema Mwenyekiti huyo wa APPT Maendeleo Mkoa wa Mbeya na kutumia salamu za imani za dini akisema;

"Ukienda msikitini huwezi sema Bwana Yesu Asifiwe, utasema Asalam Alaykum, ukienda kanisani utasema Bwana Yesu asifiwe na sio asalam, hapo utapokelewa umekuwa sehemu yao."

Wapo pia wenye kuwanyoshea kidole viongozi, wakiwalaumu kutolifanyia kazi la vurugu za vijana kwa mantiki ya kulichunguza na kuibuka na utatuzi wa kudumu.

"Ni kitu gani kimepungua hadi vijana wawakatae viongozi wao, wafanye utafiti kujua tatizo ni nini," anasema mkazi wa Jiji la Mbeya, Daimon Mwasampeta, kisha anaongeza akisema; "Hawa vijana wako mitaani humu, kulikuwa na viwanda, vyote vimekufa, vijana wako mitaani."

Miongoni mwa maeneo yenye kuathiriwa na vurugu za mara kwa mara mkoani humo ni yenye mikusanyiko mikubwa, yakiwemo maeneo muhimu ya kibiashara kama vile Mwanjelwa, Uyole na Mbalizi na vituo vya mabasi, maeneo ambayo sehemu kubwa yametawaliwa na vijana.

RC Kandoro azungumza
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro analiangalia tatizo la fujo hizo kwa jicho la hadhari, hata hivyo akiwatupia mzigo viongozi wa vyama vya siasa mkoani humo kutekeleza wajibu wao.

"Mimi ni muumini wa sheria za nchi, ni wajibu wetu kuzitii sheria zilizotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)," anasema Kandoro.
Mkuu huyo wa mkoa, anawasihi viongozi wa vyama vya siasa mkoani Mbeya kuwaelemisha wafuasi wao kutii sheria na kanuni zinazosimamia uchaguzi wakizingatia kuwa wamekubaliana, na anabainisha hilo akisema;

"Tumewaambia wasimamizi wa uchaguzi wawaite viongozi wa vyama vya siasa na kuwaeleza kuacha vitendo vya fujona waheshimu makubaliano yao."
Akizungumzia tukio la Jumapili, Kandoro alisema ni vurugu zilizosababishwa na kikundi kidogo cha vijana ambacho hakukuwa na sababu hata ya kutumia nguvu.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa Mkoa, hatua ya Dk Magufuli kuwasalimia na kuongea nao ilitosha kumaliza munkari ya vijana hao ambao baadaye nao walionekana kukubaliana naye nakumshangilia ikiashiria kukubaliana naye.

Hata hivyo Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi, Jimbo la Mbeya Mjini, Musa Zungiza alieleza kutokuwa na taarifa ya tukio hilo akisema hafahamu chochote.
"Ningeweza kulizungumzia kama kungekuwa na mkutano wa kampeni, lakini kama mtu amepita tu sidhani kama nahusika," alisema Zungiza.

Tukio la Jumapili sio la kwanza kutokea tangu kuanza kwa kampeni za uchaguzi mkoani Mbeya, ambapo tukio la kwanza likihusisha wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) jijini humo kupita eneo la mkutano wa CCM wakiwa kwenye magari wakiwa na bendera, picha za wagombea wao na kupiga kelele, wakati mgombea wa nafasi ya urais kupitia CCM, Dk Magufuli akiendelea na mkutano, jambo linaloelezwa kuwa kinyume cha makubaliano ya vyama.

Tukio la pili lilihusisha wafuasi wa CCM kushambulia msafara wa mgombea ubunge wa Chadema, Jimbo la Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi wakidai wamepita kwenye eneo lao la mkutano.

Wakati wa uzinduzi wa kampeni za ubunge za CCM, Jimbo la Kyela, wafuasi wa Chadema walishambuliwa na wafuasi wa CCM baada ya kuvamia eneo hilo la mkutano na kusimika bendera za chama chao kinyume cha makubaliano ya vyama vya siasa.

Baadhi ya viongozi wa vyamavya siasa waliozungumza na gazeti hili walionya dhidi ya vurugu hizo wakibainisha kuwa itakapofikia hatua ya wafuasi wa kila chama wakajipanga kuendesha vurugu za kuwazomea wenzao pale wanapopita, basi hakutakuwa na amani tena.

"Hivi ikitokea na upande wa pili nao wakaamua kuhamasisha vijana wao kuzomea wapinzani wao kwenye mikutano yao au wanapopita, itakuwaje," anahoji kiongozi mmoja wa jiji hilo akiwashangaa viongozi wa vyama vya siasa kukaa kimya wakiviona kuwa ni vya kawaida.

Chanzo Raia Mwema

0 comments:

Post a Comment