Wednesday 30 September 2015

Re: [wanabidii] Lowassa akikumbuka kutubu, atasema na hili

kama chanzo ni Raia Mwema, unarudia hapa ili nini? Kwani watu ni malofa hata gazeti hawanunui?



On Wednesday, September 30, 2015 11:14 PM, 'francis kinyawela' via Wanabidii <wanabidii@googlegroups.com> wrote:


Pamoja na yote hayo nakumbuka Mh Lowassa ndiye aliyeaamuru fedha zilizokuwa kwenye Fixed Deposit account ya Manispaa ya Ilala takribani milioni mia mbili zikajenge shule za Kata. Sijui kama kuna Mh. mwingine alisema hivyo.


From:"'lang'itomoni lokomoi' via Wanabidii" <wanabidii@googlegroups.com>
Date:Wed, Sep 30, 2015 at 22:18
Subject:[wanabidii] Lowassa akikumbuka kutubu, atasema na hili


Lowassa akikumbuka kutubu, atasema na hili

KWA muda mrefu nimekaa kimya kusikiliza watu wakizungumza, na hasa mgombea urais kupitia Chadema anayeungwa mkono na vyama vinne, vya NCCR-Mageuzi, CUF na NLD chini ya umoja wao maarufu kwa jina la Ukawa, Edward Lowassa, na wapambe wake kuhusu ujenzi wa shule za sekondari za kata.

Kinachozungumzwa ni kwamba Lowassa ndiye mwanzilishi wa shule hizo huku baadhi ya vijana wenye umri kati ya miaka 18 hadi 23, wakitangaza kuwa bila Lowassa wasingepata nafasi.

Vijana hao wanafikiri hivyo kwa madai kuwa ni Lowassa ndiye aliyekuna kichwa kubuni wazo hilo la kuanzishwa kwa shule za kata ambazo wana Ukawa walipokuwa katika Bunge la Tisa na hata la 10 walikuwa wakiziita shule za yeboyebo kwa madai kuwa hazifai kwa lolote lakini baada ya Lowassa kuingia Ukawa, sasa ni kete yao
kisiasa.

Maneno ya Lowassa na wapambe wake kuwa ndiye aliyefanya kazi hiyo ni kupotosha ukweli na kufuta historia halisi ya nani hasa mbunifu wa wazo hilo, mwezi Machi mwaka 2006.

Chimbuko la shule za kata
Kiini cha wazo la kuanzishwa kwa shule za kata kinahusisha historia ndefu tangu utawala wa awamu ya kwanza chini ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kupitia tume ya kupitia mfumo wa elimu ya Tanzania aliyoiunda Novemba, mwaka 1980, na kuanza kazi rasmi mwanzoni mwa mwaka 1981.

Tume hiyo ilijulikana kama Tume ya Jackson Makweta, kama Mwenyekiti na Katibu wake alikuwa ni Musel Muze, na miongoni mwa wajumbe wa tume hiyo ni pamoja na maprofesa watatu na wajumbe wengine takriban tisa.

Sitaki kwenda kwa undani kuhusu kazi au hadidu rejea za tume hiyo kwa leo, lakini mojawapo ya mapendekezo ya msingi yaliyozaa wazo la kuanzishwa kwa shule za kata ni taarifa ya tume hiyo iliyokuwa na kurasa 354 nje ya viambatanisho, iliyolenga kufanyia marekebisho mfumo mzima wa elimu wa nchini, kwa kupanua kwanza elimu ya sekondari.

Katika mapendekezo hayo mojawapo ya hatua iliyopendekezwa na Tume ya Makweta ni kuhakikisha kwamba ifikapo mwaka 1985, kila tarafa iwe na shule ya sekondari na baadaye kila kata ziwe na shule ya sekondari. Pia tume ilipendekeza baada ya miaka mitano, yaani mwaka 1990 upanuzi wa elimu ya juu uanze rasmi kwa kasi.

Katika pendekezo hilo, Tume ya Makweta iliitaka serikali kupandisha 'ngazi' vyuo vya ufundi vilivyokuwa maarufu kipindi hicho kama Dar Tec, Arusha Tec, Mbeya Tec, Musoma Tec kuwa vyuo vikuu, ili kuongeza nafasi ya elimu ya juu na kufanya Tanzania iendane na mataifa mengine katika elimu ya juu.

Kwa kuwa wakati huo kulikuwa na chuo kikuu cha umma kimoja tu, Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM) na tawi lake dogo la Morogoro, tume pia ilipendekeza tawi hilo lipanuliwe kuwa chuo kikuu kinachojitegemea kazi ambayo ilizaa matunda ya kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), mwaka 1984.

Yapo mengi yaliyojiri katika taarifa ya Tume ya Makweta iliyowasilishwa kwa Rais Julius Nyerere, mwezi Machi mwaka 1982, ikiwamo kuhakikisha Kiswahili na Kiingereza ndizo ziwe lugha rasmi za kutumia kufundisha katika ngazi zote ili kuwezesha Tanzania kwenda sawa na mataifa mengine. Kwa kuwa sitaki kujadili kazi na utekelezaji wa tume, kwa ujumla sitakwenda mbali zaidi ya hapo kwa kuwa iko siku nitaandika juu ya utekelezaji wa maoni ya tume hiyo kwa wakati muafaka.
Mkapa na mapendekezo ya ya Makweta

Alipoingia madarakani Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, mwaka 1995 alianza kutekeleza kwa vitendo maoni ya Tume ya Makweta kwa kubuni Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) na Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES).

Kwa wale wanaojua watakumbuka kuwa MMEM ililenga kupanua nafasi za shule za msingi na kuboresha mazingira ya shule ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa vitendea kazi huku MMES, pia ikiwa na lengo hilo kwa shule za sekondari.

Ili kutekeleza azma yake kwa ufanisi mkubwa Rais Mkapa kama kiongozi wa nchi alielekeza kuwepo kwa awamu ya kwanza ya mipango hiyo yaani MMEM na MMES, ambapo awamu ya pili iliangukia katika serikali ya awamu ya nne.
Kikwete na ujenzi wa shule za kata

Baada ya Serikali ya Awamu ya Tatu kukamilisha kazi yake na kukabidhi kijiti cha kuongoza nchi kwa Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kiwete, Novemba 2005, Edward Lowassa aliteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, huku Waziri wa Elimu akiteuliwa Magareth Sitta na Naibu wake akiwa Mwantumu Mahiza (wote hao wakiwa ni walimu).

Mwezi Machi mwaka 2006 kulifanyika mkutano wa watendaji wa serikali katika Hoteli ya Blue Peal, Ubungo jijini Dar es Salaam.

Katika mkutano huo, kama ilivyo kwa ratiba ya wakubwa Lowassa baada ya kufungua mkutano husika iliwadiwa wakati wa kunywa chai, Naibu Waziri wa Elimu Mahiza, alifanya kile kinachoitwa ujasiri kwa kumwomba Waziri Mkuu wakati huo kumsikiliza kidogo ili amweleze shida yake kwa niaba ya waziri wake.

Katika maeelezo yake Mama Mahiza alimwambia Lowassa kuwa; "Sisi katika Mkoa wa Dar es Saalam tuna shida, tuna watoto waliofaulu lakini hawana nafasi ya kuendelea na masomo sasa tunaomba kutoa wazo la kuwapatia nafasi lakini inahitaji ushauri wako mheshimiwa."

Baada ya maelezo hayo na ufafanuzi wa kina kidogo, Lowassa alimtaka Waziri na timu yake kufika ofisini kwake kesho yake saa nane mchana ili wamweleze kwa undani ni mikakati gani waliyokuwa nayo kuhakikisha watoto hao wanaendelea na elimu ya sekondari, baada ya kufaulu lakini hawawezi kusoma kutokana na ufinyu wa nafasi za sekondari kipindi hicho.

Nataka niweke wazi kuwa wakati huo, Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na shule za sekondari za serikali tatu tu. Leo mkoa huo una shule za sekondari 112.
Ufaulu ulikuwa ni watoto 33,775 sawa na asilimia 71.2 kati ya 47,459 waliofanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2005 ufaulu uliotokana pia na maboresho ya MMEM huku MMES yakiwa bado hayajatekelezwa vya kutosha kwenda sambamba na ongezeko la ufaulu.

Kati ya wanafunzi 33, 775 waliofaulu ni watoto 25,457 tu ndio waliopata nafasi ya kuendelea na masomo hivyo kufanya wanafunzi 8,300 kukosa nafasi ya kuendelea na masomo. Sitaki kueleza kwa undani mjadala uliokwepo kabla ya Mahiza kumvaa Lowassa kuhusu hali hiyo lakini nitagusia tu kwa ufupi.

Kabla ya Naibu Waziri Mahiza kumvaa Lowassa, aliwaita wabunge watatu wa majimbo kupitia CCM Mkoa wa Dar es Salaam ambao wote bado wapo, Abbas Mtemvu Jimbo la Temeke, Iddi Azan Jimbo la Kinondoni na Mussa Azan Zungu Jimbo la Ilala, na kuwaambia hali halisi kuwa watoto zaidi ya 8,000 wamefaulu lakini wamekosa nafasi ya kuendelea na elimu ya sekondari na hapo, Mahiza akawaeleza kuwa atamvaa Lowassa kumpa wazo la kuondokana na tatizo hilo.

Jibu la Lowassa kwa Mahiza
Baada ya maelezo hayo ya Mahiza kwenye chai, walipotoka hapo walikwenda moja kwa moja kujifungia ofisini yeye na wataalamu karibu wote wa ngazi ya juu hadi usiku wa manane, na kuingia tena alfajiri kwa ajili ya kuandaa kile ambacho Waingereza wanakiita "paper" ya kwenda kwa Waziri Mkuu Lowassa saa nane mchana.

Takwimu zinaonesha kuwa saa 8 kamili mchana Magret Sitta, Mahiza na watalamu wao walitinga kwa Lowassa kuwasilisha paper ya nini tatizo na ni nini wanachotaka kufanya kukabiliana na tatizo.

Walichowasilisha kwa Lowassa
Kwanza walitoa takwimu za ufaulu wa wanafunzi wa shule za msingi kwa nchi nzima wakiainisha kila mkoa kuanzia waliofanya mtihani, waliochaguliwa kuendelea na elimu ya sekondari na waliokosa nafasi kutokana na ukosefu wa shule za sekondari.

Pili walitoa takwimu maalumu kwa Mkoa wa Dar es Salaam peke yake kutokana kuwa na idadi kubwa zaidi huku serikali nzima ikiwa katika Jiji hilo kubwa Afrika Mashariki. Walitumia mfano wa Dar es Salaam kutaka kujenga hoja yao ambayo kiini chake kilikuwa ni Mahiza kutaka kufanya mambo mawili.

Jambo la kwanza alilopendekeza Mahiza kwa Lowassa ni kuomba kubadilishwa kwa sheria ili Wizara ya Elimu na Ufundi iruhusiwe kutumia fedha za MMES awamu ya pili (MMES 2) kujenga shule mpya za sekondari kwa haraka ili wanafunzi wote waliokosa nafasi waendelee na masomo badala ya fedha hizo kutumika kuboresha shule za zamani na kuwalipia ada watoto wanaotoka katika kaya masikini.

Pili alipendeleza wananchi wachangie kufyatua matofaili na kukusanya mawe, halmashauri za wilaya zichangie usafiri huku serikali kuu kupitia MMES 2 ikipeleka fedha kwa ajili ya mabati, saruji na misumari kukamisha madarasa hayo.

Wakati huo MMES awamu ya pili ilikuwa na lengo la kujenga shule 1,600 katika kipindi cha miaka mitano nchi nzima hatua ambayo bado isingesaidia kutatua tatizo kubwa lililokuwa limekumba taifa kwa wakati huo licha ya idadi hiyo kuwa ndogo mno kwa mahitaji ya nchi.

Mahiza alipata ujasiri huo kwa kuwa wakati huo alikuwa amemaliza kujenga shule ya sekondari ya sayansi kuanzia kidato cha tano hadi cha sita, ikiwa na vitu vyote Bagamoyo, kwa mfumo wa ushirikiano kati ya serikali na wananchi hivyo alikuwa na uzoefu kuhusu kile alichopendekeza kwa Lowassa.

Shule kama hiyo aliyojenga Mahiza zilitakiwa kujengwa katika kanda zote 11 za
elimu nchini japo leo sitaki kujadili kama zipo kweli au imebakia hiyo ya Mahiza peke yake.

Kutokana na 'paper' hiyo Lowassa aliguswa na mpango huo na kutoa ruhusa kwa Wizara ya Elimu kuanza kutekeleza mpango huo japo ilimchukua muda mrefu kumwelewa Mahiza.

Kwa ufupi huo ndio mwanzo wa ujenzi wa shule za sekondari za kata, sasa swali langu la msingi hapa ni je, kati ya Mahiza kwa maana ya Wizara ya Elimu na Lowassa, nani aliyeanzisha shule za sekondari?

Nataka Lowassa atuambie ukweli kuhusu hili na akiwa kama mkristo mzuri atubu katika hili. Lakini pia awaombe radhi Watanzania kwa kujitwalia sifa isiyomhusu bila kuwataja wahusika wakuu.

Lowassa angesema kuwa yeye ni miongoni mwa watendaji wa serikali walioshiriki kuhimiza ujenzi huo wala isingekuwa shida na wala nisingediriki kushika kalamu yangu inayopatika kwa nadra siku hizi kutokana na kubanwa na majukumu mengine ya kitaifa, kuandika juu ya hili.

Najua, natambua na nasema wazi kuwa mwaka 2007 baada ya Bunge la mwezi wa pili, Lowassa kama Waziri Mkuu alimsaidia Rais Kikwete kuratibu mgawanyiko wa mawaziri wote nchi nzima kusimamia uamuzi wa Wizara ya Elimu kuhakikisha shule hizo za kata zinakamilika na watoto wote waliofaulu kupata nafasi ya kuendelea na masomo wanapata fursa hiyo.

Uamuzi huo pia ulitokana na malalamiko kutoka kwa wabunge wengi kuwa watoto wamefaulu hawana pa kwenda, mimi nilikuwepo bungeni na anayenipinga akachukue hansard (kumbukumbu rasmi) za Bunge na orodha ya waandishi wa habari waliokuwapo wakati huo bungeni.

Lakini nikimnukuu Lowassa na mpambe wake namba mbili Frederick Sumaye, ambaye alikuwa waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miaka 10, alisema wazi kuwa hakuwa na nguvu ya kufanya lolote ndio maana walishindwa
kufanya mabadiliko wanayotaka sasa.

Sasa swali langu kwa Lowassa kama kweli hiyo ndio hali halisi kumbe hata usimamizi wa mawaziri kwenda mikoani ilikuwa amri ya Rais Kikwete na si yeye?
Na kama sivyo basi yeye Lowassa na Sumaye watueleze wazi kuwa kama walikuwa na mamlaka makubwa ya kuanzisha vitu kama hivyo na vikafanikiwa kumbe yale yote wanayodai walishindwa ilikuwa ni uzembe wao, hivyo Lowassa hafai kuwa Rais kwa kuwa alishindwa?

Na kama sivyo basi, mafanikio ya shule za kata tumpe Mwantumu Mahiza/ Wizara ya Elimu na Rais Kikwete kama kiongozi wa nchi, aliyetoa kibali cha kubadilishwa kwa sheria, taratibu na kanuni za matumizi ya fedha za MMES -2. Mimi nasubiri Ikulu ya sasa kabla ya kuingia Rais mpya, basi Rais Kikwete ampe Mahiza tuzo ya ubunifu na kutekeleza maoni ya Tume ya Makweta vinginevyo mnaficha ukweli wa historia.

Tusisahau kuwa moja ya pendekezo la Tume ya Makweta ambayo Mahiza alisaidia ubunifu katika utekelezaji ni upanuzi wa elimu juu yaani vyuo vikuu kuanzia mwaka 1990. Kazi hiyo imefanyika na leo kila mmoja anashuhudia nafasi ya elimu ya juu. Sasa tunapigania ubora wa elimu na si nafasi ya elimu.

Nimalizie makala yangu kwa kusema tufanye siasa kwa lengo la kuomba ushindi lakini tuwaambie Watanzania ukweli tukimhofia Mungu tunayemtaja kuwa yuko pamoja nasi kila siku, kwani iko siku tutajibu kila neno tunalotamka.

Tusisahau kuwa kadri tunavyotumia udhaifu wa Watanzania walio wengi kutojua kufanya utafiti wa mambo muhimu na kuwaaminisha uwongo kama huo kwa maslahi ya kwenda Ikulu, ndivyo tunavyozidi kubomoa taifa badala ya kujenga kwa kuwa
tutakuwa na wananchi wengi wasiojua ukweli kuhusu nchi yao na matokeo yake ni kukosekana kwa uzalendo kwa kuwa hawajui historia halisi ya mambo mbalimbali ya kimaendeleo yanayowahusu.

Siasa za uwongo, za ubinafsi kama hizi ndizo zinatufanya tuamini kuwa Kenya na Uganda wanatuzidi kwa kila kitu jambo ambalo si kweli. Nimeshuhudia mara nyingi wataalamu kutoka Kenya na Uganda wakitiririka Mamlaka ya Mawasiliamo Tanzania (TCRA) kuja kujifunza vitu na mbinu mbalimbali kuhusu uendeshaji masuala ya mawasiliano na teknolojia mpya hapa kwetu.

Nimeshuhudia vijana wa Tanzania wakibuni mbinu za kisasa jinsi ya kutumia teknolojia kama Maxmalipo inayoongoza, lakini leo ukimuuliza kijana wa Tanzania kuhusu ubunifu huo, atakwambia ukitaka kujua mambo mengi kuhusu teknolojia nenda India au Afrika Kusini. Kisa kajazwa uongo na wanasiasa wanaojitafutia ufalme. Tuache siasa za uongo tuseme ukweli, tujenge taifa madhubuti kwa maslahi yetu sote. –

Chanzo Raia Mwema
--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.


0 comments:

Post a Comment