Thursday 3 October 2013

[wanabidii] Kufungiwa kwa Magazeti ya Mwananchi na Mtanzania: Tujifunze nini?



--
"Vision is the ability to see the invisible!"
Hamisi A. Kigwangalla, MD, MPH, MBA
P.O.Box 22499,
Dar es

Kufungiwa kwa Magazeti ya Mwananchi na Mtanzania: tujifunze nini?  

Imeandikwa na Dkt. Hamisi Kigwangalla, MB.

 

Hivi majuzi Ndg. Assah Mwambene ambaye ni msemaji mkuu wa serikali na mkurugenzi wa idara ya habari maelezo alitoa tamko ambalo lilibainisha taarifa za kufungiwa kwa magazeti mawili kwa makosa ya uchochezi. Magazeti haya ni lile la Mwananchi, lililofungiwa kwa siku 14 na la Mtanzania lililofungiwa kwa siku 90. Yote haya ni magazeti makongwe na hivyo yanasomwa na watu wengi. Mimi binafsi kwa mfano, kama nitanunua gazeti moja kwa siku, basi kama siyo The Guardian basi ni lazima litakuwa ni 'Mwananchi.' Kufungiwa kwa magazeti kunayakosesha makampuni yanayoyamiliki mapato na pia yanawakosesha wasomaji taarifa. Wapigania haki za binadamu watasema hapa kuwa kuyafungia magazeti ni kuvunja misingi ya haki za binadamu za kupata taarifa na pia ni kuminya uhuru wa kupashana habari.

Tayari kuna hoja mtaani kwamba sheria ya magazeti ya mwaka 1976 iliyotumika kutoa habari hizi ni ya 'kizamani', 'imepitwa na wakati' na ingepaswa kufutwa. Kuna hoja nyingine kwamba sheria hiyo ina vifungu 18 vinavyokwenda kinyume na misingi ya haki na uhuru wa kupashana habari, ambao kimsingi unalindwa na katiba. Rafiki yangu Mhe. Zitto Kabwe (Mb.) ameiita sheria hii 'ya kidikteta' katika makala yake yenye kichwa cha habari 'Kufungiwa magazeti – wahafidhina sasa wanaongoza', na hapa namnukuu,  'sheria ya kidikteta ya magazeti ya mwaka 1976 ambayo tume ya Jaji Francis Nyalali iliiorodhesha kama sheria kandamizi.' Mwandishi nguli wa habari na vitabu, Mzee Ndimara Tegambwage wakati MwanaHALISI lilipofungiwa mwaka jana aliwahi kuiita sheria hii kuwa ni 'Draconian' akiilinganisha na sheria zilizokuwa zikitungwa na mtunga sheria wa Ugiriki ya kale aliyeitwa Draco, kwa ukali na 'ukatili' wake.  Haya ni maneno na mtazamo mkali sana dhidi ya sheria hii. Je, ulazima wa serikali kuleta mapendekezo ya sheria mpya bungeni? Ama wabunge tuibuke na kuleta miswada yetu binafsi? Ni maswali yanayohitaji majibu.

kwa vyovyote vile sheria hii ni lazima inahitaji kufanyiwa marekebisho makubwa ama hata kufutwa na kutungwa sheria mpya itakayoendana na mabadiliko makubwa ya katiba yaliyopita hapo katikati hususan yale ya mwaka 1984 yaliyoongeza vipengele vya haki za binadamu (bills of rights) na yale ya miaka ya '90.

Katika makala ya Mhe. Zitto Kabwe amekumbushia kauli ya Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete, Rais, kuwa 'kuna watu wanauchukulia uvumilivu wangu huu kama udhaifu…..nataka kutoa mfano tu kuwa tuvumiliane' na pia anatoa maelezo ya kumnukuu Rais kuwa aliwahi kusema wenzake wanamtaka 'aongeze ukali'. Nafahamu nia ya mtu makini kama Rais Kikwete kwenye nafasi ya uongozi wa juu kama huu alionao ni wazi kabisa itakuwa ni kutaka kuacha jina lake likikumbukwa kwa mazuri (legacy) na watanzania wenzake. Niweke kumbukumbu wazi kabisa hapa kwamba hakujatokea Rais aliyeruhusu uhuru wa vyombo vya habari kama huyu toka taifa hili lizaliwe. Lakini pia tumeshuhudia hakujatokea bunge lenye wabunge wanaoweza kumtukana Rais kwa 'uvumilivu' wake kama hili. Tulisikia namna Mhe. John Mnyika (Mb.) wa Ubungo alivyoamua kumtukana Rais bungeni bila sababu na kwa jeuri na ufedhuli wa hali ya juu. Kwanza Rais ni mzazi kwa Mhe. Mnyika na zaidi ni kiongozi anayeheshimika kwa mamlaka na nafasi yake kwa taifa letu, lakini katika hali ya kushangaza watanzania wengi walishuhudia Mhe. John Mnyika akimwita Rais 'names'….'akim-label' 'dhaifu' kwa huo 'uvumilivu' wake. Vyombo vya habari viliandika jambo hili vikimpamba kuwa ni mwanasiasa 'mahiri' na 'jasiri'. Hakuna chombo kilichokumbuka kuwa Rais Kikwete ameamua kuvumilia matusi yale tu. Wala hakuna chombo kilichomkanya huyu kijana mdogo tu Mhe. Mnyika kwa kumtusi Rais wetu sote!

Tukio hili lilipaswa litukumbushe kuwa hakuna uhuru usio na mipaka. Pia hakuna haki isiyo na wajibu. Binafsi suing mkono mkono wa chuma wa serikali kuiangukia tasnia ya habari nchini, hapana! Pia suing mkono mambo mengi yanayoandikwa kwenye vyombo vya habari kwa sababu za chuki binafsi za wenye vyombo hivyo ama wenye mamlaka ya kuahariri habari hizo ama waandishi wenye maslahi yao binafsi. Wasomi na wana habari kwenye nchi yoyote ile yenye watu wanaojitambua ndiyo mihimili inayoheshimika kwa kuwa na utaifa zaidi kwenye maoni yake kwenye mambo mbalimbali mazito ya kitaifa. Kuwa na maadili ya kazi ni jambo la mbele kabisa. Husani ukiwa unafanya kazi nyeti kama ya habari ama ya kufundisha watoto. Kwa sababu unakuwa na jukumu la kimaadili la kuhakikisha unalinda misingi ya taifa na tunu zake kama amani, upendo, udugu, usawa, uzalendo, utangamano wa kitaifa, umoja na mshikamano. Kuna mambo yasiyofaa kushabikiwa (kuwa glorified) na magazeti kwa mfano – uasi kwa serikali, kuanguka kwa dola, wasiwasi kwa usalama wa Taifa, jeshi la wananchi na majeshi yetu yote mengine na utengano wenye misingi ya ukanda, ukabila ama udini. Haya ni mambo ya hatari. Leo hii mtu akitukana bungeni, na haswa akiwa anaitukana serikali ataandikwa ukurasa wa mbele na baadhi ya vyombo vya habari kuwa yeye ni shujaa – kwamba hilo ndilo jambo la kuwaambia watanzania, lakini mwingine atakayechangia hoja ya kukuza uchumi wetu kupitia kilimo habari yake si mali kitu.

Vyombo vya habari ni taasisi nyeti sana kwenye taifa lolote lile. Vinaweza kujenga ama kubomoa. Wengine wanapenda kusema ni 'mhimili wan ne wa dola.' Vina kila sababu na ulazima wa kujijenga katika hadhi na heshima hiyo ya kuwa mhimili wan ne wa dola. Vinatakiwa vifahamu kuwa jukumu la kujenga taasisi yao ni la kwao wenyewe na heshima haiji bure, inakuja kwa kujiheshimu pia. Taasisi inapaswa kujenga taswira yake yenyewe kabla haijaanza kulia lia ijengewe na mtu mwingine. Kuna baadhi ya vyombo vya habari na baadhi ya wanahabari wamejishusha kiasi cha kujikuta wameingia kwenye mifuko ya watu ama vingine vinafanya kazi ya vyama ama wafadhili fulani. Hauwezi kujenga heshima yako kama unashindwa kusimamia misingi ya kimaadili midogo midogo kama hii.

Kwa vyovyote vile tunahitaji sheria mpya, ambayo tutaijadili na kukubaliana sote kwamba tunataka sheria mpya iwe na mambo gani, mfano adhabu zipi ziwekwe kwa yale magazeti yatakayokwenda kinyume na maadili kama vile kusingizia watu mambo ambayo hawakuyafanya kwa kisingizio kuwa 'eti ni mambo yanayosemwa semwa mtaani'. Kwamba mwandishi anaandika akionesha kuwa hata yeye amesikia na hivyo anaandika hivyo hivyo kwa kusikia sikia kwake. Anajua kabisa akienda mahakamani hatofungwa na sheria kwa sababu hakusema 'moja kwa moja' kuwa Fulani amefanya nini bali alisema habari ya kusikia sikia tu! Sasa tunataka sheria mpya itungwe na iweke bayana adhabu zitakazochukuliwa dhidi ya magazeti yatakayokuwa yakifanya utumbo unaofanana na huu. Mimi si mshabiki wa Sheria yoyote ile kandamizi lakini ni muumini mkubwa sana wa uwajibikaji. Atakayekosa basi na apewe adhabu stahiki yake kulingana na kosa lake. Mfano badala ya kuyafungia moja kwa moja magazeti unaweza kutengeneza utaratibu wa kuyakatia idadi ya nakala wanazoweza kuchapisha na ukadhibiti kuwa wachapishe hizo tu, lengo hapa likiwa kuwaminya kwenye mapato kwa siku kadhaa ili wajifunze. Adhabu ya kulizuia lisitoke kabisa ama kulifungia milele zinakuwa ni za juu kabisa. Na kabla ya kufikia uamuzi huo wanapaswa wawe wanajua kosa lao na adhabu zake, na wasikilizwe na jopo maalum litakalosimamia utoaji wa adhabu hiyo, siyo kuachia mamlaka yote kwa mtu mmoja tu, Waziri wa Habari, kama ilivyo sasa.

Dkt. Hamisi Kigwangalla, MB ni Mbunge wa Jimbo la Nzega na pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI). Ni mhitimu wa Digrii ya Udaktari wa Tiba za Binadamu, Shahada za uzamili kwenye Afya ya Jamii (MPH) na kwenye Usimamizi wa Biashara (MBA). Kwa sasa anaandika tasnifu yake ya digrii ya Uzamivu(PH.D.) kwenye Afya ya jamii (mifumo ya usawa na uchumi wa afya).

 

salaam.
Tanzania.
Phone No: +255 754 636963
                +255 782 636963
website: www.peercorpstrust.org or www.hamisikigwangalla.com
Email: hamisi.kigwangalla@peercorpstrust.org or info@hamisikigwangalla.com
Skype ID: hkigwangalla
Blog: blog.hamisikigwangalla.com 

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.

0 comments:

Post a Comment