Tuesday 23 October 2012

[wanabidii] Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya SSRA waota mbawa (?)

Mjadala: Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya SSRA waota mbawa (?)
23/10/2012

0 Comments


Kwenye kundi la WanaMabadiliko Tanzania, mada ifuatayo imewasilishwa na Benjamin Daudi Dotto.
Kama unataka kufuatilia, unaweza kufanya hivyo kwa kubofya hapa.
MUSWADA WA MAREKEBISHO YA SHERIA YA SSRA WAOTA MBAWA,WAFANYAKAZI WALIOACHA KAZI AU KUACHISHWA KAZI KUENDELEA KUTESEKA
Wadau,

Hatimaye msimamo wa serikali juu ya kupeleka marekebisho ya sheria ya mifuko ya hifadhi ya jamii leo umeota mbawa baada ya kuthibitishwa mbele ya kamati ya kudumu ya maendeleo ya jamii ya Bunge iliyokutana na katika ukumbi wa wizara ya maendeleo ya jamii mjini Dar es salaam kwamba wizara ya kazi na ajira haijaandaa muswada huo. Akithibitisha juu ya swala hilo wakati akitoa maelezo ya wizara mbele ya kamati,katibu mkuu wa wizara hiyo ndugu shitindi amedai kwamba wizara imejipanga kupeleka miscellaneous amendments kwa mwanasheria mkuu wa serikali.

Katika amendments hiyo katibu mkuu amesema kwamba kifungu kitakachorekebishwa ni kile Na.44 cha sheria ya PPF ambacho ndo pekee kitaruhusu wanachama wa PPF kuchukua mafao yao.Wanachama wa mifuko mingine kama NSSF fao la kujitoa halitarudishwa katika sheria hivyo kubaki wakisubiri miaka 55 au 60 kuchukua mafao yao.Katika mjadala huo hoja mbalimbali zilijitokeza,mojawapo ni ile iliyoibuliwa na bwana Benjamin Dotto.

Akitoa mchango wake bwana Dotto alitaka kujua kwa nini wizara imekaidi kutekeleza mapendekezo ya bunge la nane,ambalo kupitia kwa mbunge Jaffo liliitaka wizara kurudisha fao la kujitoa kwa wafanyakazi wanaoacha au kuachishwa kazi wakati mchakato wa marekebisho ya sheria ukiendelea.Lakini vilevile alitaka kujua kwa nini wizara imekaidi kuandaa muswada wa sheria badala yake unaleta miscellaneous ammendments.

Akiwasilisha mapendekezo ya wafanyakazi mbele ya kamati,Dotto alisema kwamba rasilimali zote na fedha zilizoko kwenye mifuko ni mali ya wanachama wa mifuko hii.Kwa hiyo ili pesa hizi ziweze kulindwa na kukaa salama,wakati umefika uendeshaji wa mifuko hii usimamiwe na wanachama wenyewe.Hivyo akapendekeza mwenyekiti wa mamlaka ya SSRA,na wenyeviti wa mifuko mingine wasiteuliwe na rais bali wachaguliwe na wanachama wa mifuko ili wakienda kinyume waweze kuwajibishwa na wanachama wenyewe.pendekezo hili lilipingwa vikali na Mustafa mkulo na wabunge wengine kwa sababu linainyima serikali nafasi ya kuteua wenyeviti hao.

Akifafanua Dotto alisema kwamba lengo kubwa la pendekezo hilo ni kuiondolea serikali mamlaka ya kutumia fedha za wanachama jinsi wanavyotaka wao,kwa mfano ujenzi wa Udom,Daraja la kigamboni na njia za mabasi yaendayo kasi ni miradi inayotumia pesa za wanachama kwa sababu wasimamizi wa mifuko hiyo ni wateule wa rais.Kauli hiyo ilimsababishia kasheshe bwana dotto kwani alizuiliwa kuendelea kutoa mapendekezo mengine maana yalionekana kugusa masilahi ya wakubwa.

Hata hivyo baadhi ya mapendekezo aliyozuiliwa kuyataja na kufafanua mbele ya kamati ni pamoja na;

.1, FAIDA INAYOPATIKANA KUTOKANA NA UWEKEZAJI WA MIFUKO HIYO IGAWIWE KWA KILA MWANACHAMA KILA MWISHO WA HESABU ZA MWAKA KWA KUWEKWA KATIKA AKAUNTI YA MWANACHAMA.

2. MWANACHAMA ARUHUSIWE KUHAMA MFUKO MMOJA KWENDA MWINGINE KWA KUHAMA NA MAFAO YAKE FAIDA NA HAKI ZINGINE.

3.MFANYAKAZI AKIACHA AU KUACHISHWA KAZI MAFAO YAKE YALIPWE NDANI YA SIKU SABA.

4. KUWEPO NA MIKOPO YA WANACHAMA NA WARUHUSIWE KUCHUKUA HADI NUSU YA MAFAO YAO,DHAMANA YA MKOPO IWE MAFAO YAKE YALIYO KATIKA MFUKO.

Kwa ufupi hayo ndo baadhi ya mambo yaliyojiri.ANGALIZO wafanyakazi bado tuna safari ndefu sana kuweza kufika kwenye nchi ya ahadi na bila MSHIKAMANO DAIMA tutabaki kutendwa na kugeuzwa na serikali kama mafungu ya nyanya kama hali halisi ilivyojidhihirisha leo.

Naomba kuwasilisha.
Mchango wa John Mnyika (Mbunge wa Ubungo)
Wadau,

Mosi, mrejesho huu unadhihirisha masuala kadhaa niliyotahadharisha wakati mkutano wa nane wa Bunge, sasa yanaanza kujidhihirisha.

Pili, kama nilivyoeleza wakati huu msingi wa tangazo la SSRA la kusitisha fao la kujitoa kwa mifuko yote haikuwa marekebisho ya sheria yaliyofanyika tarehe 13 Aprili 2012 kama walivyoeleza, bali kuna marekebisho mengine yaliyofanyika miaka mingi ambayo yalikuwa hayatekelezwi. Katika muktadha huo ikiwa kuna dhamira ya kurekebisha hali hiyo, tunapaswa kurudi mpaka nyuma.

Tatu, wakati marekebisho ya sheria yakisubiriwa ni muhimu Wizara ya kazi ikazingatia maelekezo na maelekezo ya kisera niliyohitaji yatolewe kutengea tangazo la SSRA. Itakumbukwa kwamba baada ya Waziri kueleza kuwa ataleta muswada wa marekebisho na bunge kupitisha azimio bado nilishika mshahara wa Waziri na kumtaka atoe maelezo na maelekezo, pamoja na majibu ya Waziri badala ya kutoa maelekezo ya kutengua tangazo/agizo chini kwa chini wameendelea kutoa maelekezo kwamba SSRA inyamaze kimya. Kuna nini ambacho Serikali inaona vigumu kukisema na kukifanya?

Nne, toka mwanzo wa kadhia hii nilieleza kwamba pamoja na hatua ya haraka ya kutengua agizo la SSRA ufumbuzi wa kudumu unapatikana kwenye kurekebisha sheria kwa kuwa chanzo cha tatizo lenyewe ni sheria. Maelezo binafsi au hoja binafsi ni hatua tu kupeleka kwenye marekebisho ya sheria, na tungeweza kuruka hatua hiyo kwenye mkutano wa nane wa bunge na kwenda moja kwa moja kwenye kurekebisha sheria na tatizo hili lingekuwa limeahirishwa (nasema kuahirishwa sio kumalizwa kwa kuwa kulimaliza kunahitajika mabadiliko makubwa katika mfumo mzima wa hifadhi ya kijamii nchini). Kwa mujibu wa Katiba ibara ya 63 Bunge ndio lenye kutunga sheria, bunge lingeweza lenyewe kurekebisha hiyo sheria kwa muswada wake na hatimaye Rais kusaini, bunge likapeleka tena suala hilo kwa serikali ambayo inasuasua kulitekeleza. Kwa uwajibikaji wa pamoja, nitangaze maslahi kwamba mimi ni sehemu ya bunge hilo.

Tano, tunakwendaje mbele kutoka hapa? Ieleweke kwamba suala hili sasa ni la Bunge, sio la mbunge mmoja mmoja, ingawa kila mbunge anawajibu wa kusimamia utekelezaji wa maamuzi ya bunge kwa nafsi na nafasi yake. Ni la Bunge kwa sababu kuna azimio la Bunge tayari kuwa muswada uwasilishwe mkutano wa tisa wa bunge. Hivyo, ikiwa serikali inasuasua, bunge lichukue nafasi yake na kuwasilisha muswada; inaweza kuwa kupitia muswada wa kamati husika ya bunge baada ya kupokea majibu hayo ya serikali au muswada binafsi kutoka kwa mbunge yoyote ambaye bunge litaona anaweza kuwasilisha. Hata hivyo, kwa kuwa kwa maelezo haya Serikali imesema badala ya muswada kwa hati ya dharura wa marekebisho ya sheria za hifadhi ya jamii hoja hiyo inatarajiwa kuwasilishwa kupitia marekebisho ya sheria mbalimbali hii nayo ni hatua. Ushauri wangu kwa wadau mdai yafuatayo: Waziri Mkuu Mizengo Pinda au Mwanasheria Mkuu wa Serikali mmoja wao atoe kauli hadharani kuwa serikali imebadili msimamo kutoka kauli ya Naibu Waziri Makongoro Mahanga kama ilivyonukuliwa na Gazeti la Guardian On Sunday tarehe 14 Oktoba 2012 kuwa muswada utakuja Februari 2013 kwa kupelekwa na Wizara ya Kazi na Ajira na sasa muswada utaletwa tarehe 30 Oktoba 2012 na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupitia muswada wa marekebisho ya sheria mbalimbali. Aidha, rasimu ya muswada huo (naita rasimu, kwa sababu kama ni hati ya dharura, muswada hautachapwa kwenye gazeti la serikali bali utaonekana kwa mara ya kwanza ndani ya bunge) itolewe kwenye vikao vya kamati vinavyoendelea hivi sasa na utolewe pia kwa wadau na umma kwa ujumla ili kuhakikisha marekebisho hayo hayahusu PPF pekee bali ni pamoja na NSSF nk.

Tuendelee na mjadala,

JJ
Mchango wa Weston Mbuba kwa mtindo wa maswali akimwuliza Mnyika
Mh. Mnyika, JJ, (Mb.)

Nikuulize maswali machache.

- Kwanini PPF wakaruhusiwa kunufaika na fao la kujitoa na si mifuko mingine?

- Serikali inaogopa nini kutoa mafao hayo kwa wachangiaji wa mifuko hiyo?

- Kwa uelewa wako, Bunge linaweza kuchukua hatua gani za kuhakikisha sheria hii inafutwa haraka iwezekanavyo na kuwa rais anaridhia mabadiliko hayo. Kwani Bunge linaweza kuibadili, kama ulivyosema lakini rais asiisaini na kuiidhinisha.

Kwa kanuni zenu, kuna namna yoyote ambayo rais anaweza kushinikizwa atekeleze kitu chenye maslahi kwa wananchi ilhali yeye mwenyewe hapendi?
Majibu ya Mnyika kwa Weston
Weston,

Naingia kwenye kikao lakini kwa haraka haraka:

1. Kwa nini PPF na si mifuko mingine, kwa kuwa Serikali ndio iliyokuja na mwelekeo huo inaweza kujisemea yenyewe. Lakini wanaweza kuja na maelezo kuwa awali PPF ilikuwa provident na sio pension pekee na kwamba marekebisho ya tarehe 13 April yaliyoelekezwa na Bunge yalihusu sheria hiyo pekee kwa upande wa fao la kujitoa. Maelezo hayo yasikubalike kwa sababu hifadhi ya jamii kwa mifuko yote inapaswa kutafsiriwa zaidi ya penseni ya uzeeni, kuna mafao mengine ya zaidi. Na kwamba hata baada ya marekebisho ya sheria kwa upande wa NSSF yaliyofanyika miaka kadhaa nyuma bado mafao ya kujitoa yaliendelea kutolewa (wanaweza kuja na maelezo kwamba yalikuwa kinyume cha sheria). Kama watakuja na majibu kuwa fao la kujitoa kwa NSSF lilikuwa linatolewa kinyume cha sheria maelezo hayo ni sababu tosha ya kwamba marekebisho hayo yanayoletwa pamoja na kugusa kifungu cha 44 cha sheria ya PPF yahusu pia sheria ya NSSF. Kama watakuja na majibu kuwa hakuna ulazima wa kurekebisha sheria kwa upande wa NSSF basi watoe tangazo la kutengua agizo la SSRA la kusjitisha mafao ya kujitoa kwa mifuko yote.

2. Serikali inaogopa nini kutoa fao la kujitoa? Mimi si msemaji wa Serikali, hata hivyo maelezo yanayotolewa ni kwamba fao la kujitoa si sehemu ya mafao ya msingi katika mfumo wa hifadhi ya jamii kwa mujibu wa mikataba ya ILO na hivyo kutolewa kwake kunaathiri lengo la msingi la kuwa na pensioni ya uzeeni. Majibu hayo hayana msingi, kwa kuwa hayazingatii ukweli kwamba mfumo wetu kwa sasa hauna mfumo mbadala wa kuziba pengo hilo mathalani fao la ukosefu wa ajira au fao la mkupuo kwa kuzingatia mazingira ya kazi katika sekta binafsi na hali halisi ya ujira, ajira na uchumi wetu. Pia, baadhi ya vifungu hivyo vinavyotumika kupigia upatu nchi yetu haijaridhia ndio maana hakuna ulazima wa kisheria wa mifuko yetu kutoa mafao yote tisa. Aidha, mazingira yetu ya kisera, kiuchumi na kijamii hayatufanyi tufanane na hizo nchi nyingine wanazozitolea mfano. Hivyo, majibu hayo yanayotolewa kimsingi ni visingizio, kuna majibu ambayo hayatolewi kwa uwazi juu ya mashaka kuhusu uendelevu wa mifuko pamoja na acturial studies kuonyesha kwamba mifuko yetu ni endelevu ripoti za CAG zinaonyesha kwamba kuna uwekezaji kwenye miradi isiyofanya kazi kwa ufanisi (non performing investments), unaweza pia kurejea hotuba yetu ya Kambi ya Upinzani Bungeni kupitia kwa Waziri Kivuli wa Kazi na Ajira kwa maelezo zaidi.

3. Kwa kuwa Serikali imesema inaleta muswada wa sheria ya marekebisho ya
Sheria mbalimbali, muswada ukishasomwa bungeni utakuwa ni mikononi mwa Bunge na unaweza kurekebishwa kwa kadiri ya matakwa ya wananchi. Ndio maana nasema mutake kama ni kwa hati ya dharura, serikali iweke wazi kwa umma kabla mapendekezo/rasimu ya muswada inaokusudia kuupeleka. Kama ni kwa utaratibu wa kawaida, siku 21 kabla ya Bunge zimeshafika, hivyo kama kuna muswada kama huo serikali ieleze ulichapwa kwenye gazeti la Serikali la tarehe ngapi na namba ngapi wadau muanze kuujadili.

4. Kuhusu nafasi ya Rais katika mchakato huu, naomba nisijibu chochote katika hatua ya sasa, mjadala wa sasa tupate kwanza kauli ya Waziri Mkuu Pinda au Mwanasheria Mkuu wa Serikali Werema zitatoa mwelekeo kuhusu sakata hili la fao la kujitoa kwa kuwa Wizara ya Kazi na Ajira kupitia kwa Waziri Kabaka na Naibu Wake Mahanga wameshindwa kutoa uongozi unaohitajika kumaliza mgogoro huu na wafanyakazi kwa kushughulikia chanzo kwa wakati badala ya kusubiri kukabiliana na matokeo.




Source: http://www.wavuti.com/#ixzz2A7o0SSxp

--
Karibu Jukwaa la www.mwanabidii.com
Pata nafasi mpya za Kazi www.kazibongo.blogspot.com
Blogu ya Habari na Picha www.patahabari.blogspot.com

Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma

Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.

0 comments:

Post a Comment