Sunday 16 September 2012

[wanabidii] MATUKIO YALIYOPITA YAWEFUNZO KWA WANAHABARI TANZANIA

Matukio yaliyopita yawefunzo kwa wanahabari Tanzania
Na Happiness Katabazi

SEPTEMBA 2 mwaka huu, Mwandishi wa habari wa Kituo cha utangazaji cha Chanel Ten, Daudi Mwangosi alifariki dunia katika vurugu zilizotokea katika mkutano wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), na Polisi wilayani Mufindi Mkoani Iringa.

Vyombo vya habari na waandishi wa habari waliokuwepo kwenye eneo hilo la tukio waliueleza umma kupitia vyombo vya habari kuwa ni Jeshi la Polisi ndiyo waliomua Mwangosi kwa kipigo na bomu.

Baada ya vyombo vya habari kuaminisha umma hilo, umma uliamini hilo na baadhi taasisi ya kiraia na vyama ya siasa vikatoa matamko ya kulaani mauji hayo na kulihukumu moja kwa moja kuwa jeshi la polisi ndiyo lililomua na baadhi ya vyombo vya habari vilichapisha picha iliyokuwa ikionesha askari mmoja akiwa ameshika bunduki na kumuelekezea Mwangosi na wengine walifikia hatua ya kusema huyo askari aliyeonekana kwenye picha hiyo ambaye walishindwa kumtaja jina lake ndiye aliuemua marehemu huyo.

Aikuishia hapo Jumanne ya wiki hii, baadhi ya waandishi wa habari waliandama wa mikoa kadhaa waliandamana kulaani mauaji hayo na wale wa Mkoa wa Dar es Salaam, waliandamana na kuweka mkutano pale Viwanja vya Jangwana huku wakiwa na mabango yaliyosomeka hivi 'Polisi wakaoge, polisi wauji'.

Pia walimtimua na kumtolea maneno ya kebei katika mkutano huo Waziri wa Mambo ya Ndani,Dk.Emmanuel Nchimbi kwa madai kuwa hawakumualika licha kuna taarifa za chini chini ambazo bado hazijathibitishwa zinadai kuwa miongoni mwa wahariri walimualika Dk.Nchimbi katika mkutano huo.Ni suala la muda tu ukweli utakuja kujulikana.

Kwani kwa watu tunaofikiri sawa sawa tumekuwa tukijiuliza hivi inawezekanaje Waziri Dk.Nchimbi kwa madaraka aliyonayo anawezaje kufunga ofisi yake na kuja kwenye eneo hilo bila kuarikwa?. Je waandishi waliomfikia hatua hiyo ya kumfukuza Dk.Nchimbi kwa madai kuwa siyo mwanahabari na hawajamwalika katika mkutano huo lakini ni wanahabari hao hao walimpatia nafasi Dk.Exavely Rwaitama ambaye si mwanahabari nafasi ya kuhutubia kwenye mkutano huo.

Baadhi ya wanahabari waliomtimua Dk.Nchimbi pale Jangwa na kutoa maneno ya kulipa matope jeshi la polisi wakati waliomfanyia unyama ule Mwangosi ni askari wachache ambao siyo jeshi zima, kuwa Nchimbi ni kiongozi wa nchi na amekuwa akishirikiana kwa karibu na vyombo vya habari na ujio wake pale Jangwani haukuvunja sheria zozote za nchi kwani Katiba ya Nchi inatoa haki kwa kila mtu kwenda kokote anakotaka idi mradi asivunje sheria na pia yeye ni binadamu anastahili heshima mbele ya jamii hivyo kitendo cha kumzomea wakati si yeye aliyetenda kosa hilo na tayari alikwishachukua hatua ya kuunda Kamati ya kuchunguza chanzo cha mauji hayo hakikua cha kiungwa katika jamii iliyostaharabika kwani sisi waandishi wa habari ni kioo cha jamii hivyo tunapaswa kutenda matendo, kuandika na kutangaza mambo ambayo yanastaha na kuifundisha vyema jamii.

Tendo la kumzoea Dk.Nchimbi tukae tukijua baadhi ya watoto wetu na makundi mengi wanaweza kulichukulia kuwa ni sawa na mwisho wa siku nao wanaweza kuja kumzoea kiongozi mwingine yoyote au watu wazima waliowazidi umri kwa kigezo kuwa hata wanahabari walishawahi kumzoea Waziri Nchimbi na hawakuchukuliwa hatua zozote za kinidhamu.

Kumbukeni Dk.Nchimbi ,jeshi la polisi lipo chini yake na polisi ambalo tumelihukumu kuwa limemuua mwenzetu bila hata mahakama bado haijatoa hukumu kuwa ni jeshi hilo ndilo,na ni polisi hao hao ambao leo hii tumewatoea maneno ya kuwakashfu licha jeshi hilo limeunda tume ya kuchunguza chanzo cha mauji hayo ndiyo lenye mamlaka ya kupeleza kesi za jinai hususani kesi hiyo mauji ya Mwangosi,na tukumbuke nao ni binadamu na wanamshikamano wa kweli kuliko sisi waandishi wa habari ambao kwanza hatupendani,wanauwezo pia wakutumia madaraka yao vibaya ya kupeleleza kesi kwa kualibu ushahidi na mwisho wa siku upande wa jamhuri wakashindwa kesi hiyo, hivyo mmemtukana Mamba wakati Mto hamjavuka.

Turejee kwenye mada yangu ya leo ambayo ninataka umma hususani wanahabari wenzangu tujenge utaratibu wa kujifunza kutokana na matukio mbalimbali na maamuzi mbalimbali yanayotolewa na mahakama.

Nasema hivyo kwasababu ni wazi kuwa vyombo vya habari hapa nchini tunaonekana ni watu wa kusahau matukio mapema na hatutaki kujifunza kutokana na matukio yaliyopita.

Kwani leo hii vyombo vya habari vimeuaminisha umma kuwa ni polisi ndiyo walioua Mwangosi.Lakini waandishi hao wanasahau kuwa jeshi la polisi ni taasisi na inaafanyakazi wake ambao ni polisi na watumishi raia.

Hivyo vyombo vya habari tunavyoshinikiza aliyemua Mwangosi wakamatwe na kufikishwa mahakamani bila kusema mtu anayetuhumiwa kumua Mwangosi akamatwe tunakosea kwani mwisho wa siku tukumbuke Ibara ya 13(6)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inasema; 'Ni marufuku kwa mtu aliyeshitakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu mwenye kosa hilo mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo'.

Pia tukumbuke kifungu cha 7(1)(B) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 inasema hivi; " Kila mtu analojukumu la tarifa polisi kuhusu tukio la kifo cha binadamu mwenzie cha kawaida au kilichosababishwa na vurugu au umemkuta mtu mwili wa marehemu bila kujua chanzo cha kifo chake unatakiwa ukatoe taarifa polisi".

Pia kifungu cha 10 cha sheria ya hiyo kinatoa mamlaka kwa ofisa wa polisi kupeleleza matukio ya uhalifu.Na kifungu cha 60(1) cha Sheria hiyo kinasema ofisa yoyote msimamizi wa kituo au ofisa yoyote wa mpelelezi wa makosa ana mamlaka ya kuendesha gwaride la utambuzi lengo likiwa mashahidi wa kesi inayokusudiwa kufunguliwa mahakamani waweze kumtambua mtu anayetuhumiwa kutenda kosa husika".

Kwa matakwa ya vifungu hivyo vya sheria hapo juu, ni wazi sisi waandishi wa habari hususani wale waandishi wenzetu waliokuwepo kwenye vurugu zilizosababisha Mwangosi kufariki hawajatekeleza kwa vitendo vitendo matakwa ya vifungu hivyo.

Yaani hawajaenda kutoa taarifa za kifo hicho kwenye kituo cha polisi wala kwa ofisa wa polisi, hawajaitwa kwenye gwaride la utambuzi kumtambua mshitakiwa aliyetenda kosa hilo la mauji hadi Septemba 12 mwaka huu, Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk.Eliezer Feleshi kumfikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa, askari mwenye namba G2573 Pasificus Cleophace Simoni (23).Ambapo wakili wa Serikali Michael Lwena alidai mshitakiwa huyo anakabiliwa na kosa la mauji ya Mwangosi na kifungu cha 196 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.



Nawakumbusha waandishi wenzengu tuache kuongea sana bila kuitenda na kujifunza,tuongee na kuandika kwa kuwa na vielelezo ambavyo mwisho wa siku vitaisaidia mahakama kuwatia hatiani watuhumiwa wa makosa mbalimbali.

Leo hii tunasema kabisa ni polisi ndiyo walioua lakini tunashindwa kutaja jina la polisi aliyeua.Nisisi waandishi waandishi wa habari enzi zile za tukio la mauji ya wafanyabiashara wanne wa wilayani Mahenge mkoani Morogoro.Tulishupalia na kushikia bango kuwa ni polisi na aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaa,Abdallah Zombe ndiyo waliowaua wafanyabiashara hao bila ya kuwa na ushahidi na mwisho wa siku Mahakama Kuu chini ya Jaji wa Mahakama ya Rufani hivi sasa Salum Massati aliwaachiria huru kwa maelezo kuwa jamhuri imeshindwa kuthibitisha kesi hiyo na akalitaka jeshi la polisi likawatafute wauaje na kwamba Zombe na wale washitakiwa wenzie siyo wauaji wa wafanyabiashara wale.

Na baada ya kuachiriwa huru Zombe aliyashitaki baadhi ya magazeti likiwomo gazeti la Uhuru, Tanzania Daima, Dar Leo kwa madai kuwa lilimhukumu kabla hajahukumiwa na kesi zipo mahakamani isipokuwa gazeti la Uhuru lilikwenda kumwomba msamaha Zombe na hatimaye Zombe akaiondoa kesi hiyo mahakamani wakaenda kumalizana nje ya mahakama.

Pia ningali nikikumbuka tukio la uvamizi katika ofisi za gazeti la Mwanahalisi ambapo watu wasiyojulikana walimjeruhi Mwandishi Saed Kubenea na Ndimara Tigambwage na sisi waandishi wa habari na jamii kwa ujumla tulifanya maandamano na kupiga kelele kutaka wahusika wakamatwe wafikishwe mahakamani na kweli polisi iliwafikisha mahakamani watuhumiwa hao pale Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Oktoba 2012 ,mahakama hiyo iliwaachilia huru kwa madai kuwa jamhuri imeshindwa kuleta ushahidi wa kuthibitishia mahakama kuwa ni kweli washitakiwa hao ndiyo waliyemjeruhi Kubenea na Ndimara.

Tukio jingine ni kuhusu mkataba wa kampuni ya kufua umme ya Richmond, tuliandika na kufikia hatua ya kujipa mamlaka ya kusema mkataba huo uliingiwa kwa misingi ya Rushwa na kuandika makala za kumdhihaki Mkurugenzi Mkuu wa (TAKUKURU), Dk.Edward Hosea ambaye alisema hakukuwa na tuhuma za rushwa katika mkataba huo na mwisho wa siku DPP-Dk.Feleshi alimfikisha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mfanyabiashara Naeem Gile aliyekuwa akitetewa na wakili wa kujitegemea Alex Mgongolwa kwa makosa ya kutoa taarifa za uongo kuhusu kampuni hiyo ya Richmond, lakini mwaka jana Hakimu Mkazi Waliarwande Lema, alimwachiria huru baada ya kumuona hana kesi ya kujibu.

Tukio jingine ambalo sisi wanahabari,wanasiasa na waharakati ni lakupinga hukumu ya mahakama ya kimataifa ya ICC, iliyoipa kampuni ya Dowans Tanzania, tuzo ya dola za kimarekani milioni 56, ambapo tulisema ni rushwa na haiwezekani la mwisho wa siku Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilikubali tuzo hiyo isajiliwe hapa nchini na wiki iliyopita mahakama hiyo tena ilitupilia mbali ombi la Tanesco lilokuwa linataka mahakama itoe amri ya kuzuia utekelezwaji wa hukumu ya mahakama kuu ya Tanzania iliyoruhusu tuzo hiyo ya Dowans isajiliwe.

Kwa mifano hai hiyo hapo juu, nataka kuwaasa sisi wanahabari tusiwe watu wenye kasumba ya kupayuka payuka bila kuwa na ushahidi kwani tukumbuke yale tunayoyaandika ndiyo umma wanayoyaamini na kuyafuata.

Pia kama tunaandika fulani ni muuaji,mla rushwa bila ya kuwa na ushahidi na hilo tukae tukijua wananchi wengi wanaamini hivyo.Na kama tunaandika hivyo basi tuakikishe tunakwenda pia kutoa taarifa hizo za Fulani ni mharifu kwenye mamlaka husika ili ziweze kufanyiwa kazi kwani matukio hayo ya kesi hizo yamenifundisha kuwa sisi waandishi na umma tunapenda sana kuamini vitu vya kusikia bila kuwa na ukweli na ushahidi thabiti ambao kama ushahidi huo tungewapelekea waendesha mashitaka wetu wangeweza kuutumia kuijenga kesi yao kwani ikumbukwe kuwa Kifungu cha 90(1) cha Sheria ya Makosa ya Jinai, inaeleza majukumu ya DPP na moja ya jukumu lake ni kuendesha kesi za jinai mahakamani kwaniaba ya serikali.

Na DPP huyo huyo ndiyo mwenye madaraka ya kugawanya madaradaka yake kwa mawakili hao wa serikali kwenda mahakamani kwaniaba yake kuendesha kesi za jinai kama ilivyo kwenye kesi hiyo ya mauji ya Mwangosi ambapo DPP,anawakilishwa na Lwena.

Sasa wakili huyo aweze kufanya miujiza yoyote ya kushinda kesi hiyo kama mashahidi wa kesi hiyo hawatailetea vielelezo na ushahidi kwa polisi ili yeye aweze kuviwasilisha mahakamani.Na tukumbuke sisi waandishi wa habari kama tunataka mauji kwa wanahabari wenzetu na raia wenzetu wasiyona hatia licha siwezi kusema nini kilisababisha waliompiga na kuumua Mwangosi nini kwasababu sijui nini kilisababisha wampigie hadi kuumua , nilazima tuwe wepesi wa kushirikiana na polisi na waendesha mashitaka kwa kupeleka ushahidi mzuri ambao utaifikisha mahakama iwaone washitakiwa wanahatia.

Aidha nawaasa baadhi ya waandishi wa habari wenzangu tusimame kwenye maadili ya kazi yetu,tusiingize hisia na mapenzi ya vyama kwenye kazi kwani mwisho wa siku tunaoumia ni sisi na siyo hao viongozi wa vyama wala watoto wao wala wake zao kwani kwenye maandamano haramu viongozi hao hawaji na wake zao na watoto ila wakati wanaapishwa kushika madaraka viongozi hao wa siasa ndiyo uenda na wake zao na ndugu zao kwasababu huko hakuna virugu vya polisi.

Kwani hata Mwenyekiti wa Baraza la Habari (MCT), Kajubi Mkajanga wiki, hii amewataka waandishi wa habari kuacha kuwa wasemaji wa vyama siasa jambo ambalo binafsi namuunga mkono Mkajanga kwani hivi sasa baadhi ya waandishi hapa nchini wanaingiza mapenzi ya vyama vyao,na urafiki wa baadhi ya viongozi katika taaluma jambo ambalo linachafua heshima ya taaluma hii ambayo ni muhimu sana katika kuliletea maendeleo taifa letu. Naomba kutoa hoja.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika

0716 774494

Chanzo:www.katabazihappy.blogspot.com ; Septemba 16 mwaka 2012.

--
Karibu Jukwaa la www.mwanabidii.com
Pata nafasi mpya za Kazi www.kazibongo.blogspot.com
Blogu ya Habari na Picha www.patahabari.blogspot.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
 
 

0 comments:

Post a Comment